1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchaguzi waingia dosari Afrika ya kati

Admin.WagnerD5 Januari 2016

Wagombea 20 wanaowania nafasi ya uraisi katika uchaguzi mkuu katika Jamuhuri ya Afrika ya kati uliofanyika wiki iliyopita wametaka kusimamishwa kwa zoezi la kuhesabu kura wakidai kuna ukiukwaji mkubwa wa taratibu.

https://p.dw.com/p/1HY5I
Wapiga kura Jamuhuri ya Afrika ya Kati wakiwa katika msitari kuelekea kupiga kura.
Wapiga kura Jamuhuri ya Afrika ya Kati wakiwa katika msitari kuelekea kupiga kura.Picha: Getty Images/AFP/I. Sanogo

Wagombea hao walitoa kauli hiyo katika mkutano na waandishi wa habari hapo jana mnamo wakati karibu asilimia 40 ya kura zilizopigwa zikiwa tayari zimekwisha hesabiwa.

Katika taarifa yao ya pamoja wagombea hao walisema kulikuwa na ukiukwaji wa taratibu uliombatana na vitisho wakati wa zoezi hilo la uchaguzi ambao ulifanyika Desemba 30 mwaka jana na kutaka zoezi zima la kuhesabu kura lisimamishwe .

Wagombea hao wametaka pande zote muhimu zinazohusika katika kusimamia uchaguzi huo kukutana haraka kwa mazungumzo ili kuweza kulikwamua taifa hilo katika hali hiyo ya sasa.

Msomi katika taaluma ya Hesabu aongoza

Hatua hiyo inakuja mnamo wakati mgombea huru wa nafasi ya uraisi katika uchaguzi huo Faustine Archange Touadera, ambaye ni waziri mkuu wa zamani wa nchi hiyo akiongoza kwa kiasi kikubwa ambapo amejizolea asilimia 23 ya kura ambazo tayari zilikuwa zimekwishahesabiwa.

Waziri mkuu wazamani wa Jamuhuri ya Afrika ya Kati Faustine Faustine Archange Touadera.
Waziri mkuu wazamani wa Jamuhuri ya Afrika ya Kati Faustine Faustine Archange Touadera.Picha: Getty Images/AFP/I. Sanogo

Mgombea huyo ambaye ni msomi aliyebobea katika masuala ya hesabu katika ngazi ya Uprofessor awali hakupewa nafasi kubwa ya kuibuka mshindi miongoni mwa wagombea wanaowania nafasi ya uraisi katika uchaguzi huo.

Anicet Georges Doguele ambaye pia ni waziri mkuu wazamani alikuwa akifuatia katika nafasi ya pili katika kura hizo wakati Desire Kolingba mtoto wa Rais wazamani wa nchi hiyo akishika nafasi ya tatu.

Nafasi ya nne ilichukuliwa na Jean-Serge Bokasa mwenye umri wa miaka 43 ambaye ni mtoto wa mtawala wa zamani wa taifa hilo katika kipindi cha kuanzia mwaka 1966 hadi mwaka 1979 aliyepata karibu kura 34,000 ya kura hizo ambazo zimekwishahesabiwa.

Waziri mkuu mwingine wazamani Martin Ziguele na anayeonekana kuwa chaguo la Ufaransa ambayo ndiyo iliitawala nchi hiyo wakati wa kipindi cha ukoloni alikuwa anafuatia katika nafasi ya tano akipata kura 28,000.

Kuna uwezekano wa hatua ya pili ya uchaguzi huo kuitishwa hapo January 31 mwaka huo.

Mapinduzi yalimuweka madarakani Michel Djotodia.

Jamuhuri ya Afrika ya kati ambayo ni moja ya mataifa masikini ulimwenguni na yenye historia ya utawala wake kupinduliwa ilitumbukia katika vurugu zilizokuwa na mrengo wa kidini mwaka 2013 mnamo wakati aliyekuwa Rais wa nchi hiyo Francois Bozize alipoondolewa madarakani katika mapinduzi yaliyoongozwa na muuungano wa waasi wa kiisilamu yaliyomuweka madarakani Michel Djotodia ambaye alikuwa rais wa kwanza muisilamu katika taifa hilo.

Rais wazamani wa Jamuhuri ya Afrika ya Kati Michel Djotodia.
Rais wazamani wa Jamuhuri ya Afrika ya Kati Michel DjotodiaPicha: Reuters

Maelfu ya raia wa taifa hilo waliuawa huku wengine wakilazimika kukimbia makazi yao katika vurugu za kidini zilizohusisha makundi ya kikiristo na waisilamu.

Umoja wa mataifa na Ufaransa ulilazimika kuingilia kati mwaka 2014 il kurejesha amani katika taifa hilo hatua iliyopelekea kuondolewa madarakani kwa kiongozi huyo wa kiisilamu Michel Djotodia kufuatia shinikizo la kimataifa.

Karibu watu milioni mbili kwenye taifa hilo lenye watu karibu milioni tano walitarajiwa kupiga kura katika uchaguzi huo.

Mwandishi: Isaac Gamba/ AFPE/APE

Mhariri: Josephat Charo