1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchomaji wa Koran washutumiwa duniani kote

Sekione Kitojo9 Septemba 2010

Mpango wa kuchoma nakala za kitabu kitakatifu cha Waislamu cha Koran katika jimbo la Florida nchini Marekani umezusha shutuma kali duniani kote

https://p.dw.com/p/P84e
Mchungaji Terry Jones wa kanisa la , Dove World Outreach Center mjini Gainesville, Florida. ambaye anapanga kuchoma nakala za Koran ifikapo Septemba 11.Picha: AP

Mpango  wa  kuchoma  nakala  za  kitabu  kitakatifu  cha Waislamu  cha  Koran   katika  jimbo  la  Florida  nchini Marekani  umezusha  shutuma  kali  duniani  kote.

Mkuu  wa  masuala  ya  kigeni  wa  umoja  wa  Ulaya Catherine  Ashton  ameshutumu  kwa  jumla  tukio  hilo linalopangwa,  ambapo  mkuu  wa  jumuiya  ya  nchi  za Kiarabu  Amr Mussa  amemueleza  mkuu  wa  kanisa  hilo mchungaji  Terry  Jones   kuwa  ni  shabiki  tu,  na kuliambia  shirika  la  habari  la  AFP  kuwa  anawataka Wamarekani  kupinga  vikali  hatua  kama  hiyo.

Kituo   cha  kanisa  linaloongozwa  na  mchungaji  Jones kinachojulikana  kama " njiwa  anayewafikia  watu  wote duniani ", cha  mjini  Gainesville, Florida  kimeapa kuchoma  nakala  za  Koran  wakati  wakiwakumbuka  kiasi watu  3,000  waliouwawa  na  watu  walioteka  nyara  ndege kutoka  katika  kundi  la  Al-Qaeda.

Baraza  la  Kikatoliki  linalohusika  na   madahalo  baina  ya dini  limesema  katika  taarifa  kuwa , kila  dini, pamoja  na vitabu  vyake  vitakatifu  na  alama  zake , ina  haki  ya kuheshimiwa  na  kulindwa.

Rais  Barack  Obama  amezungumzia   kwa  mara  ya kwanza   leo  kuhusiana  na  mpango  huo  wa   mchungaji kutoka  Florida  kutaka  kuchoma  nakala  za  Koran , akisema  kuwa  itakuwa  ni  bahati  kubwa  kwa  al-Qaeda, na  kumuomba   mchungaji  huyo  kubadili  mawazo  yake.

Lakini  akijibu  miito  ya  maafisa  wa  ngazi  ya  juu  wa mambo  ya  kigeni  kutoka  India, Pakistan  na  kwingineko kuwa  serikali  ya  Marekani  inapaswa  kuzuwia  kuchomwa kwa  nakala  hizo, Obama  amedokeza   katika  mahojiano na  shirika la  habari  la  ABC  kuwa   mikono  yake imefungwa  na  katiba  ya  Marekani.

Mchungaji  huyo  Terry  Jones, anaweza  kutajwa  tu  kuwa alifanya  tukio  hilo, Obama  amesema. Jones  na  kundi lake  dogo  la  waumini   katika  mji  wa  Gainesville , wanapanga   siku  ya  Jumamosi  kufanya  kumbukumbu ya  mwaka  wa  9  wa  shambulio  la  kigaidi  dhidi  ya Marekani   kwa  kuharibu  kitabu  hicho  kitakatifu   cha Waislamu. Halmashauri  ya  jiji  hilo  imekataa  kumpa kibali  cha  kuchoma  moto, na  unajitayarisha  na  hatua za  usalama  kwa  ajili  ya  tukio  hilo.  Kamanda  wa majeshi  ya  NATO  nchini  Afghanistan  jenerali  David Petraeus  ameonya  kuwa   kuchoma  nakala  za  Koran kutatoa  nafasi  kwa  propaganda  ya  wapiganaji  wa Taliban.

"Tuna  wasi  wasi  kuwa  picha  za  kuchoma nakala  za Koran , zitatumiwa  kwa  njia  ile  ile, kama  wale  watu wenye  msimamo  mkali  wa  kidini  walivyotumia  picha  za jela  ya  Abu  Ghraib. Kwa  maana  nyingine  picha  hizo zitakaa  milele  katika  mtandao  na  zitatumiwa  na  wale ambao  hawatutakii  mema  kuchochea  ghasia   na   hasira miongoni  mwa  watu  wa  kawaida  dhidi  yetu  na  ujumbe wetu  hapa  Afghanistan  pamoja  na  ujumbe  mwingine duniani.

Viongozi  wa  kidini  wa  Marekani   pamoja  na  watu wengine, wanapanga   kwenda  Gainesville  kupinga uchomaji  wa  Koran.

Katika  miongo   ya  hivi  karibuni, mahakama  kuu  ya Marekani  imeweza  kutoa  haki  kwa  Wamarekani   hata kuchoma  bendera  ya   nchi  hiyo  kama  tukio  la  uhuru wa  kujieleza  unaolindwa   chini  ya  katiba  ya  Marekani.

Wizara  ya  mambo  ya  kigeni  ya  Marekani  imezitaka balozi  zake  zote  nje  ya  nchi   kufanya  mikutano  na kutathmini  hatari  wanayokabiliana  nayo  Wamarekani , iwapo  kanisa  hilo  nchini  Marekani  litakaidi  maoni  ya dunia  na  kuchoma  nakala  hizo  za  Koran.

Mwandishi : Sekione  Kitojo / DPAE/ AFPE

Mhariri : Mohammed  Abdul Rahman