1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ufalme wa Saudi Arabia watoa rambirambi, kifo cha Khashoggi

Zainab Aziz
22 Oktoba 2018

Ufalme wa Saudi Arabia umetoa rambirambi kwa familia ya mwandishi habari Jamal Khashoggi, aliyeuwawa ndani ya ubalozi mdogo wa falme hiyo mjini Istanbul, huku kadhia hiyo ikizidi kuuandama.

https://p.dw.com/p/36w1D
Saudi Arabien Mohammed bin Salman
Picha: picture-alliance/AP Photo/C. Owen

Utawala wa kifalme nchini Saudi Arabia mapema leo ulitoa rambi rambi zake kwa familia ya mwandishi habari Jamal Khashoggi aliyeuawa kwenye ubalozi wake mdogo huko mjini Istanbul,Uturuki. Mrithi wa ufalme wa Saudi Arabia Mohammed bin Salman amezungumza na mtoto wa Khashoggi kwa njia ya simu.

Mfalme Salman pia ametoa rambirambi kwa familia ya mwandishi huyo wakati ambapo taifa hilo linaendelea kushinikizwa kimataifa hata baada ya kukiri mnamo siku ya Jumamosi kwamba mwandishi wa habari wa gazeti la Marekani la Washington Post aliuawa ndani ya ubalozi wake mnamo tarehe 2 Oktoba katika mazingira ambayo mpaka sasa bado sababu zinazotolewa zinakinzana.

Mwandishi wa habari Jamal Khashoggi
Mwandishi wa habari Jamal Khashoggi Picha: picture-alliance/AA/O. Shagaleh

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan amesema maelezo kuhusu mauaji ya Khashoggi yatafunuliwa kinaga ubaga bila kificho. Erdogan aliyasema hayo alipolihutubua bunge.

Waziri wa mambo ya nje wa Indonesia Retno Marsudi amesema kwenye mkutano wake na waziri wa mambo ya nje wa Saudi Arabia Adel al Jubeir kwamba rais wa Indonesia Joko Widodo, anataka uchunguzi wa wazi na wa kina ufanyike.

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan
Rais wa Uturuki Recep Tayyip ErdoganPicha: picture-alliance/AP Photo/T. Kovacs

Jamii ya kimataifa inaendelea kuitilia shaka Saudi Arabia kutokana na ufafanuzi wake kuhusu kifo cha mwandishi wa habari Jamal Khashoggi. Viongozi mbali mbali ulimwenguni wanataka maelezo kamili juu ya mahali ulipo mwili wa mwandishi huyo. Umoja wa Ulaya, Australia, Kanada na Umoja wa Mataifa zimeisisitizia Saudi Arabia itoe maelezo zaidi.

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel ametoa wito wa kuzingatiwa uwazi, akiongeza kuwa taarifa zilizopo juu ya kile kilichotokea katika ubalozi wa Istanbul hazitoshi. Kansela Merkel amesema Ujerumani imesimamisha mauzo ya silaha kwa Saudi Arabia kwa muda na amezitaka nchi nyingine za Ulaya kufuata mfano huo.

Mwandishi.Zainab Aziz/APE/AFPE/p.dw.com/p/36uso

Mhariri:Mohammed Abdul-Rahman