1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yajipanga kushughulikia masuala ya wakimbizi

Sudi Mnette
6 Novemba 2023

Kuongezeka kwa idadi ya wakimbizi kumeiweka serikali ya Ujerumani katika hali ya shinikizo na kwa sasa taifa hilo la Ulaya linapanga kuongeza hatua za kuwarejesha kwao waomba hifadhi ambao maombi yao yamekataliwa.

https://p.dw.com/p/4YRTC
Waziri wa Mambo ya Ndani Ujerumani Nancy Faeser
Waziri wa Mambo ya Ndani Ujerumani Nancy FaeserPicha: LISI NIESNER/REUTERS

Kuongezeka kwa idadi ya wahamiaji na wakimbizi ikilinganishwa na hatua ya idadi ndogo ya wanaorudishwa makwao limekuwa suala kubwa la kisiasa nchini Ujerumani, huku wafuasi wa mrengo wa kulia wakitumia hali hiyo katika upingaji wa wa wahamiaji.

Kansela Olaf Scholz alitangaza sera kali zaidi ya ukimbizi katika mahojiano yake na jarida la Spiegel la Ujerumani, ambapo nikimnukuu anasema "Hatimaye lazima tuwaondoshe kwa kiwango kikubwa wale ambao hawana haki ya kusalia Ujerumani."

Aliendelea kwa kusema haiwezekani kabisa kuwa taratibu za kuwarejesha watu hao mara zote zichukue muda miaka mingi.

Kama ilivyo kwa Kansela, Waziri wa Mambo ya Ndani Nancy Faeser, kutoka chama cha Social Democrat, anataka kutekelezwa kwa ahadi hiyo na amewasilisha mswada ambao umeidhinishwa na baraza la mawaziri la shirikisho.

Soma pia:UN: Takriban watu milioni 4.4 duniani hawana uraia wowote

Aliwaambia waandishi wa habari mjini Berlin kwamba mageuzi ya taratibu za uhamisho ilikuwa ni hatua moja tu katika mfululizo wa sera za uhamiaji.

"Tunahakikisha kwamba watu wasio na haki ya kuishi Ujerumani wanapaswa kuondoka nchini kwetu haraka zaidi." Alisema.

Aliongeza kwamba "Kwa njia hii, tunaimarisha uungaji mkono wa jamii kwa ajili ya kupokea wakimbizi nchini Ujerumani."

Alisema hatua za kuzuia, kuhakikisha urejeshwaji zaidi na wa harakani muhimu ili Ujerumani iweze kutimiza wajibu wake wa kibinadamu kwa wale wanaohitaji ulinzi dhidi ya vita na ugaidi.

"Kulinda haki ya msingi ya hifadhi, ni lazima tuweke kikomo uhamiaji usio wa kawaida," alisema waziri Nancy.

Mamalaka yapewa nguvu zaidi

Miongoni mwa mambo ambayo yameainishwa katika mswada wa waziri Faeser ni pamoja na kutoa nguvu zaidi kwa mamlaka katika kuwarejesha watu makwao, na hasa wahalifu na wale wanaoingizwa kwa namna haramu.

Ujerumani: Rasimu ya kuwarudisha watu katika mataifa yao

Mamlaka haitawaarifu tena mapema wanaotakiwa kurejeshwa makwao kuhusu safari zao, isipokuwa familia zilizo na watoto wadogo.

Katika hali ambapo mtu anayehusika anaishi katika makazi ya pamoja na watu wengine, polisi wataruhusiwa kuingia na kupekua vyumba vingine toafuti na chumba cha kulala cha mtu huyo.

Kwa mujibu wa mamlaka, mara nyingi watu wamekwepa kuondoshwa nchini kwa kujificha katika makazi ya pamoja.

Soma pia:Uhamiaji Umoja wa Ulaya bado suala tete

Kanuni nyingine inasema ikiwa mtu au mshukiwa hana pasipoti ya kuonyesha, mamlaka pia wataweza kupekua simu yake ya mkononi  au kabati ili kubaini utambulisho wake.

Kipindi cha juu zaidi cha kumweka muhusika kizuizini kabla ya kumsafrisha kitaongezwa kutoka siku 10 hadi 28 ili kuwapa mamlaka wakati zaidi wa kujiandaa kwa safari.

Mwisho kabisa wanachama wa makundi ya uhalifu wa kupangwa nchini Ujerumani wanaweza kufukuzwa nchini, bila kujali kama wamepatikana na hatia ya uhalifu.

Kansela Scholz akutana na wakuu wa majimbo

Kansela Olaf Scholz leo atakutana na viongozi wa majimbo yote 16 ya Ujerumani kutafuta njia za kukabiliana idadi kubwa ya wahamiaji,suala ambalo limekuwa tatizo kubwa la kisiasa kwa serikali yake.

Katika mkutano huo Kansela anakabiliwa na shinikizo kubwa la kutoa majibu kuhusu suala hilo.

Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz
Kansela wa Ujerumani Olaf ScholzPicha: Kenzo Tribouilliard/AFP

Mawaziri wakuu wa serikali za majimbo wanaitaka serikali kuu mjini Berlin iongeze bajeti kwa serikali zao kushughulikia gharama za kuwapokea wahamiaji. 

Soma pia:Uhamiaji Umoja wa Ulaya bado suala tete

Makaazi ya kuwaweka wahamiaji na wakimbizi yamefurika nchini Ujeremani na Kansela Scholz anayekabiliwa na shinikizo kubwa kutoka upande wa upinzani na kwengineko akitakiwa kusitisha mpango wa kuwapokea wakimbizi,amesema wahamiaji wengi zaidi wataingia Ujerumani.

Wakimbizi zaidi ya milioni mojakutoka Ukraine waliingia Ujerumani tangu Urusi ilipoanzisha vita nchini humo.

Hali ya wakimbizi Ujerumani

Ujerumani imetoa hifadhi ya milioni moja wanaotafuta ulinzi kutokana na vita vya Urusi dhidi ya Ukraine. 

Wahamiaji wakiwa katika foleni ili kusajiliwa
Wahamiaji wakiwa katika foleni ili kusajiliwaPicha: CHRISTOF STACHE/AFP

Mbali na hilo, baadhi ya watu 244,000 kutoka nchi nyingine waliomba hifadhi kwa mwaka uliopita ambapo kwa mwaka huu pia idadi hiyo inaweza kuongezeka hadi kufikia watu 300,000.

Soma pia:Mataifa ya EU yajaribu kupata makubaliano kuhusu wahamiaji

Kwa mujibu wa Wizara ya Mambo ya Ndani, hadi mwisho wa Septemba, kulikuwa na karibu watu 255,000 wanaoishi Ujerumani ambao wanapaswa kuondoka, kati yao karibu 205,000 wana "hadhi ya kuvumiliwa" (Duldung), ikimaanisha kinadharia analazimika kuondoka nchini lakini hawezi kufukuzwa.

Lakini pia hadi mwishoni mwa Septemba watu 12,000 wamerudishwa makwao.