1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uingereza huenda ikaomba muda zaidi wa mchakato wa Brexit

Zainab Aziz
5 Oktoba 2019

Waziri Mkuu wa Uingereza Boris Johnson ameahidi kwamba atauomba Umoja wa Ulaya kuongezewa muda wa mchakato wa Brexit kwa mujibu wa Sheria ya bunge ikiwa masharti yatatimizwa.

https://p.dw.com/p/3QlMc
Großbritannien London | Wideraufgenommene Parlamentssitzung: Boris Johnson
Picha: Reuters/Parliament TV

Kwa mujibu wa hati ya mahakama ya nchini Scottland, huenda Waziri Mkuuu wa Uingereza Boris Johnson akaomba muda zaidi wa mchakato wa Brexit ikiwa makubaliano na Umoja wa Ulaya hayatafikiwa hadi kati kati ya mwezi huu wa Oktoba. Hati hiyo ya serikali iliyokaririwa na mahakama ya juu ya Scottland inaonyesha kwamba Waziri Mkuu Johnson anakusudia kufuata sheria iliyopitishwa na bunge la Uingereza inayomtaka waziri mkuu huyo auombe Umoja wa Ulaya kuahirisha tarehe ya Uingereza kujiondoa kutoka kwenye jumuiya hiyo ifikapo tarehe 31 mwezi huu. Hata hivyo hati hiyo ya mahakama inapingana na msimamo wa Johnson kwamba hataomba muda zaidi asilani. 

Wakati huo huo Jumuiya ya Ulaya imekataa ombi la serikali ya Uingereza la kutaka mazungumzo yaendelee  hadi mwishoni mwa wiki. Gazeti la Times la Uingereza limemnukuu mwanadiplomasia mmoja wa Umoja  wa Ulaya akisema, ikiwa wajumbe wataendelea na mazungumzo hadi mwishoni mwa wiki itaoonekana kama wajumbe hao wanakutana kwa vikao rasmi wakati ambapo zinahitajika juhudi zaidi ili kufikia hatua hiyo.

Mwandishi Zainab Aziz

Mhariri: Josephat Charo