1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yapambana kuokoa makubaliano ya Iran

Iddi Ssessanga
9 Juni 2019

Huku Marekani ikitishia vita katika Ghuba ya Uajemi, waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Heiko Maas anafanyakazi kunusuru makubaliano ya nyuklia ya Iran. DW inaangazia ziara yake, na wadau tofauti na malengo yao.

https://p.dw.com/p/3K6X0
Außenminister Maas mit Aiman al-Safadi in Jordanien
Picha: picture-alliance/dpa/AP/R. Adayleh

Kwa nini sasa?

Hatari ya vita katika Ghuba ya Uajemi inamtia kishindo kila mmoja. Katika muda wa miezi iliyopita, utawala wa rais wa Marekani Donald Trump umeimarisha vikwazo vyake dhidi ya Iran kama sehemu ya kampeni yake ya "shinikizo la juu kabisaa".

Washington imedai kuwa Iran inapanga mashambulizi dhidi ya maeneo ya Marekani katika kanda hiyo na kuituhumu kwa kuhusika na mashambulizi dhidi ya meli nne za mafuta nje ya pwani ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).

Marekani imeimarisha uwepo wake wa kijeshi katika kanda na kuwaondoa wengi wa wanadiplomasia wake kutoka Iraq.

Wakati huo huo, "uvumilivu wa kimkakati" wa Iran unazidi kupungua: Kufikia Julai 7, Tehran haitajifunga tena kuheshimu masharti yote ya makubaliano ya nyuklia ya mwaka 2015, ikiwa mataifa ya Ulaya hayatakuwa na mkakati makhusisi wa kuivutia Iran kiuchumi ili kusalia kwenye makubaliano hayo licha ya vikwazo vya Marekani.

Bayern - Bundesaußenminister Maas mit Mohammed Dschawad Sarif
Waziri Heiko Maas akiwa na mwenzake wa Iran Javad Zarif.Picha: picture-alliance/dpa/T. Hase

Picha kubwa pia inahusisha shambulizi lililofanywa na waasi wa Kihouthi nchini Yemen, wanaoungwa mkono na Iran, dhidi ya miundombinu muhimu ya kimkakati nchini Saudi Arabia, hasimu mkuu wa kikanda wa Iran.

Ni yepi malengo yawaziri wa mambo ya nje wa Ujermani?

Katika muafaka na Uingereza na Ufaransa, mataifa mengine yaliosaini makubaliano hayo, waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Heiko Maas anajaribu kuishawishi Iran kusalia katika makubaliano hayo.

Makubaliano hayo yanayojulikana rasmi kama Mpango Mpana wa Pamoja wa Utekelezaji (JCPAOA), yalianza kutekelezwa 2015 kufuatia majadiliano magumu.

Mjini Tehran, Maasa atashinikiza "utulivu, busara na kupunguza mzozo," alisema msemamaji wa wizara ya mambo ya nje siku ya Alhamisi. Maas atajaribu pia kuishawishi Iran kuachana na makataa yake ya Julai 7 kwa mataifa ya Ulaya.

Maas atafanya ushawishi hasa kwa ajli ya kuruhusu muda zaidi wa INSTEX - mfumo wa malipo ulioanzishwa mwanzoni mwa mwaka na Uingereza, Ufaransa na Ujerumani ili kuepuka  vikwazo vya Marekani - kuwa na ufanisi.

Hata hivyo, hata kama INSTEX itafanya kazi, Maas hawezi kuyalaazimisha makampuni ya Ujerumani kuwa na uhusiano wa kibiashara na Iran; bado yanahofia kukabiliwa na vikwazo vya Marekani katika njia moja.

Berlin Bundesaußenminister Heiko Maas trifft US Außenminister Pompeo
Waziri Maas (kulia), akiwa na mwenzake wa Marekani Mike Pompeo mjini Berlin, Mei 31, 2019.Picha: Imago Images/photothek

Maas alizungumza na mwenzake wa Marekani, Mike Pompeo, wakati wa ziara ya Pompeo mjini Berlin wiki iliyopita.

Marekani ilikuwa tayari imekasirishwa na maandamalizi ya Jens Plötner, mkurugenzi wa kisiasa wa wizara ya mambo ya nje ya Ujerumani, kusafiri kwenda Tehran, na inakosoa juhudi za Ulaya kujaribu kuokoa makubaliano ya nyuklia.

Ziara ya Maas mjini Tehran, ya kwanza kufanywa na waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani katika kipindi cha miaka 2 1/2, haionekani kuangaliwa vyema na Washington.

Nini anaweza kutarajia Maas mjini Tehran?

Iran inatafuta njia za kivitendo kutoka kwenye mtego wa Marekani. Inaichukulia kampeni ya "shinikizo la juu kabisaa" kama vita ya kiuchumi ambayo tayari imesababisha hasara kubwa: Mauzo ya mafuta ya Iran yameshuka, na thamani ya sarafu ya Iran, rial, imeporomoka kwa theluthi mbili tangu vikwazo viliporejeshwa mwaka uliyopita.

Mfumuko wa bei unazidi kuongezeka, na wakati chakula na dawa kimsingi haviko kwenye orodha ya vikwazo, kutengwa kwa Iran kutoka kwenye mfumo wa kifedha wa dunia kumesababisha upungufu.

Hali hiyo kwanza ya yote imewanufaisha wenye msimamo mkali katika utawala wa Iran, ambao tayari walionya mwaka 2015 kwamba mataifa ya Magharibi hayawezi kuaminika.

Iran Atomanlage Natans
Kituo cha uutubishaji urani cha Nantaz kilichopo kusini mwa Tehran, Iran.Picha: Getty Images/M. Saeedi

Ziara ya Maas mjini Tahran inafanyika wakati kukiwa na shinikizo kubwa na matarajio kidogo ya matokeo thabiti, licha ya shirika la kimataifa la atomiki (IAEA) kuhitimisha hivi karibuni kwa mara nyingine kwamba Iran ilikuwa inatekeleza masharti yake ya mkataba wa nyuklia.

Mapema wiki hii, msemaji wa wizara ya mambo ya nje wa Marekani alikataa kujadili mada zisizohusiana na makubaliano, kama vile jukumu la Iran katika kanda au programu yake ya makombora ya masafa marefu, akizielezea kama "zisizo na umuhimu."

Ni upi msimamo wa Marekani?

Hivi karibuni Trump ametoa matamshi yanayoashiria maridhiano, akibainisha kwamba hatafuti kubadilisha utawala nchini Iran au kutaka vita, lakini yuko tayari kwa mazungumzo. Pia alishusha kimya kimya malengo ya sera yake ya vikwazo, akisema sasa anataka tu kuizuwia Iran kutengeneza bomu la nyuklia.

Katika muktadha huu, rais wa Marekani anatofautiana na mshauri wake wa usalama wa taifa John Bolton, ambaye kwa miaka mingi amekuwa akitaka kubadilishwa kwa utawala mjini Tehran. Bolton pia amechangia pakubwa kuongezeka kwa mzozo katika Ghuba.

Mei 5, alizungumzia msitari mwekundu kwa hatua ya kijeshi, akisema kwamba shambulio lolote dhidi ya maslahi ya Marekani au washirika wake litakabiliwa na nguvu usiokoma, huku akishindwa kueleza bayana maslahi hayo ni yepi na ni washirika hao wa Marekani ni wepi.

Waangalizi wana wasiwasi kwamba Trump anaonekana kuwa kitu pekee kilichopo kati ya Bolton na vita na Iran.

Nini kinaweza kufuatia?

US-Präsident Trump mit Sicherheitsberater John Bolton
Waangalizi wanahofu kuwa kilichosalia kati ya Bolton na vita na Iran ni rais Trump.Picha: Getty Images/C. Somodevilla

Baada ya kutumwa kwa meli kubwa ya kubeba ndege za kivita na mashambulizi, juhudi mbalimbali za kidiplomasia hivi sasa zinafanyika.

Baada ya kuondoka kwa Maas, waziri mkuu wa Japan Shinzo Abe atasafiri kwenda Iran kufanya upatanishi katika juhudi za kidiplonasia ambazo Trump amezikaribisha.

Iraq na Oman, ambazo zina uhusiano imara na Iran na Marekani, pia zitajaribu kufanya upatanishi.

Malengo yao makuu yanapaswa kuzifanya Marekani na Iran kushiriki mazungumzo ya moja kwa moja. Lakini hili halitotokea bila Marekani kuondoa baadhi ya vikwazo vyake.

Katika kipindi cha muda mrefu, kutakuwa na utulivu wa kikanda tu ikiwa kutakuwa na makubaliano juu ya mfumo wa usalama wa pamoja unaokidi maslahi ya wadau wote wanaoshiriki, zikiwemo Saudi Arabi na Iran, ambazo zinawania kuwa na ushawishi zaidi katika kanda.

Mwanzoni mwa Juni, waziri wa mambo ya nje wa Iran Javad Zarif alitangaza kuwa nchi yake iko tayari kwa mazungumzo na Riyadh.

chanzo: dw