1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yasisitiza taifa la Israel kuwa na haki ya kuwapo

Sekione Kitojo
26 Aprili 2018

Katika mwaka ambao Israel inasherehekea miaka 70 ya kuundwa kwa taifa hilo, bunge la Ujerumani limesisitiza haki ya taifa hilo la Kiyahudi kuwapo na imeshutumu chuki dhidi ya Wayahudi nchini Ujerumani.

https://p.dw.com/p/2wjwx
Deutschland Bundestag Plenum
Picha: picture-alliance/dpa/M. Kappeler

"Haki  ya  Israel  kuwapo  na  usalama  wake  ni mambo ambayo  hayawezi  kujadiliwa  nasi,"   hoja  iliyopitishwa kwa  idadi  kubwa  ya  wabunge  wa  bunge  la  Ujerumani imesema  hii leo.

Mswada  huo  pia  umeshutumu  ongezeko  la  uhalifu unaofanywa  kutokana  na  chuki  dhidi  ya  Wayahudi nchini  Ujerumani. "Haiwezekani  kwamba  idadi  ya mashambulio   inaendelea  kuongezeka  na  kwamba Wayahudi  nchini  Ujerumani  wanajihisi kuwa  katika hatari," umeeleza  muswada  huo.

Bundestag Berlin trägt Kippa
Wabunge wa bunge la Ujerumani wakivalia kippa kuonesha mshikamano na WayahudiPicha: picture-alliance/dpa/M. Kappeler

Hoja  hiyo  iliidhinishwa  na  wabunge  kutoka  katika vyama ndungu  vya  kihafidhina  vinavyoongozwa  na kansela  Angela  Merkel , washirika  wao  katika  serikali  ya mseto  nchini  Ujerumani  chama  cha  Social Democratic Union, SPD , chama  cha  kijani, Free Democrats FDP pamoja  na  chama  mbadala  kwa  Ujerumani  AfD.

Chama  cha   siasa  kali  za  mrengo  wa kushoto cha  Die Linke  kilijiondoa  kupiga  kura  wakati  hoja  ya  ziada ambayo wanachama  wake  waliuandika  pamoja  na chama  cha  Kijani  ilikataliwa.  Chama  cha  Die Linke hakikujumuishwa   katika  kuandika  hoja  hiyo  ya  serikali ambayo  hatimaye  ilipitishwa.

Kulikuwa  na  hali  ya  kutupiana  maneno  wakati  wa mjadala wakati   kiongozi  wa  kundi  la  wabunge  wa chama  cha  Kijani  Katrin Goering-Eckardt alipokataa msimamo  wa  chama  cha  siasa kali  za  mrengo  wa  kulia cha  AfD  kwamba  chuki  dhidi  ya  wayahudi  sio  kitu  cha kweli; pia  alimueleza  kiongozi  wa  kundi  la  wabunge  wa chama  hicho Alexander gauland  kuwa  ni "chui  aliyevaa ngozi  ya  kondoo."

Deutschland Berlin - Bundestag Plenarsitzung: Alexander Graf Lambsdorff
Kiongozi wa kundi la wabunge wa chama cha FDP bungeni Alexander Graf LambsdorffPicha: picture-alliance/dpa/M. Kappeler

Vyama vyalumbana

Kiongozi  wa  kundi  la  wabunge  wa  chama  cha  FDP Alexander Graf Lambsdorff aliwashutumu  baadhi  ya wanachama  wa  chama  cha  Die Linke  kwa  kuunga mkono  kampeni  ya  vuguvugu  ambalo  liliisusia Israel pamoja  na  biadhaa  za  Israel  likijulikana  kama Susia, kutoweka  vitega  uchumi  na  vikwazo BDS.

Mbunge  wa  chama  cha AfD  Beatrix von Storch ameishutumu  serikali  ya  Ujerumani  kwa  kuchochea  kile alichosema  kuwa  ni  chuki  dhidi  ya  Israel  katika mashariki  ya  kati  kwa  kuchangia  fedha  katika  shirika  la Umoja  wa  Mataifa  linalotoa  misaada   na  kazi  kwa wakimbizi  wa  Palestina , UNRWA.

Hapo  jana  Wajerumani  wa   dini mbali  mbali  walivaa kofi  za  vibandiko  vinavyovaliwa  na  wayahudi  na  kuingia mitaani  katika  maandamano yaliyofanyika  katika  miji mbali  mbali wakipinga  shambulio  la  chuki  dhidi  ya Wayahudi  na  kuelezea  hofu  yao  juu  ya  kuongezeka kwa  chuki  dhidi  ya  Wayahudi  nchini  Ujerumani.

Muslima mit Kippa bei Demonstration gegen Antisemitismus
Maandamano mjini Erfurt , watu wa imani zote za kidini waliandamana kuunga mkono WayahudiPicha: picture-alliance/dpa/J. Meyer

Maandamano  hayo  ya  Kippa , kibandiko  yalizuka kutokana  na  shambulio  la  mchana  kweupe wiki  iliyopita lililofanywa  dhidi  ya   vijana  wawili  waliovalia kofia  hizo za vibandiko  katika  kitongoji maarufu  katika  mji  mkuu wa  Ujerumani , Berlin.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / dpae / ape

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman