1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujumbe wa Marekani kuzungumza na utawala wa kijeshi Niger

Saumu Mwasimba
19 Aprili 2024

Ujumbe wa Marekani wa maafisa wa ngazi za juu unatarajiwa kuitembelea Niger wiki ijayo ambako utafanya mazungumzo na utawala wa kijeshi wa nchi hiyo.

https://p.dw.com/p/4ezRf
Niger | Abdourahamane Tchiani
Kiongozi wa kijeshi wa Niger, Jenerali Abdourahamane Tchiani.Picha: ORTN/Télé Sahel/AFP/Getty Images

Ujumbe huo unatarajiwa kujadili kuhusu ushirikiano na kutowa mapendekezo thabiti kwa utawala huo wa mjini Niamey ya kujaribu kuimarisha mustakabali wa ushirikiano wao.

Utawala wa Niger uliyafuta makubaliano ya kijeshi na Washington mara tu baada ya kuingia madarakani mwaka 2023.

Soma zaidi: Vifaa vya kisasa vya kijeshi vya Urusi vyawasili Niger

Ziara hiyo inafuatia ile iliyofanywa mjini Washington wiki hii na Waziri Mkuu wa Niger Ali Mahamane Zeine.

Siku ya Jumanne waziri mkuu huyo alikutana na maafisa wa wizara ya mambo ya nje ya Marekani na kujadili kuhusu kuimarisha mahusiano ya kidiplomasia, kiuchumi, kibiashara na kiteknolojia.

Marekani ilisitisha takriban mahusiano yake yote ya ushirikiano ikiwemo wa kijeshi na Niger baada ya kutokea mapinduzi nchini humo.