1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UNESCO: Ziwa Turkana liko hatarini

Daniel Gakuba
29 Juni 2018

Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni UNESCO limeliorodhesha ziwa Turkana miongoni mwa maeneo yaliyoko katika hatari

https://p.dw.com/p/30X5N
Lake Turkana National Parks
Picha: AFP/Getty Images/Y. Chiba

Kamati ya shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni UNESCO jana ililijumuisha Ziwa Turkana ambalo ni muhimu sana nchini Kenya na eneo linalojumuishwa kati ya maeneo ya chimbuko la binadamu, katika orodha ya turathi zinazokabiliwa na hatari ambapo wataalamu hao waliokutana Bahrain wameonesha kwamba athari za bwawa la Ethiopia zinaongeza kitisho katika eneo hilo.

Ziwa Turkana ambalo liko kaskazini magharibi mwa Kenya na ambalo pia linajulikana kama Bahari ya Jade ni ziwa lenye kiwango kikubwa cha madini ya Seline katika eneo la Afrika Mashariki na pia ni ziwa kubwa la jangwani duniani.

Eneo hilo kwa upande mwingine lina uwezekano wa kuwa chimbuko la binadamu likiwa na sehemu zenye mabaki na mifupa katika eneo la Koobi Fora, mashariki mwa fukwe za Ziwa Turkana.

Shirika hilo la UNESCO linasema eneo hilo la Koobi fora lililosheheni mabaki ya viumbe mbali mbali limetowa mchango mkubwa zaidi katika uelewa wa mazingira yanayomzunguka binadamu kuliko eneo jingine lolote duniani.