1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Upinzani Kongo wagoma kuwasilisha pingamizi mahakamani

Saleh Mwanamilongo
2 Januari 2024

Wagombea uchaguzi nchini Kongo wana siku mbili kuwasilisha malalamiko yao kwenye mahakama ya katiba. Lakini upinzani ambao unapinga matokeo umesema hautokwenda mahakamani.

https://p.dw.com/p/4an9t
Wagombea tisa wa uchaguzi wa Kongo wapinga matokeo ya uchaguzi na wagoma kuwasilisha pingamizi mahakamani
Wagombea tisa wa uchaguzi wa Kongo wapinga matokeo ya uchaguzi na wagoma kuwasilisha pingamizi mahakamani

Mgombea wa upinzani Moise Katumbi ambaye alitangazwa kushika nafasi ya pili ya matokeo ya uchaguzi wa rais anatarajiwa kuzungumza Jumanne. Hadi sasa haijulikani ni mwelekeo upi atakaochukuwa baada ya Rais Tshisekedi kutangazwa mshindi wa uchaguzi huo. Kisheria wagombea wana masaa 48 tu ili kuwasilisha malalamiko yako kwenye Mahakama ya Katiba. Na mahakama lazima ichunguze migogoro hiyo ndani ya siku saba.

''Udanganyifu uliopangwa vyema''

Tayari msemaji wa chama cha ''ENSEMBLE pour la Republique'' cha Katumbi, Hervé Diakiese, amesema hakuna ishara yoyote ya mgombea wao kwenda kortini kupinga matokeo ya uchaguzi.

''Tulichokiita machafuko ya uchaguzi kwa hakika yalikuwa udanganyifu uliopangwa vyema na uliolenga kuleta mkanganyiko. Leo hii mbali na kambi ya Felix Tshisekedi, hakuna mtu makini, hakuna asiyeegemea upande wowote anayeweza kuridhika na kilichofanyika, na kukiita kama uchaguzi wa kuaminika.'', alisema Diakiese. 

Upinzani umesema Mahakama ya Katiba ni chombo cha rais Felix Tshisekedi ambacho hakitawatendea haki. Hata hivyo changamoto kuu kwa wagombea ni kutoa ushahidi kuunga mkono madai yao kwamba waliibiwa kura.

Kwa sababu ni vigumu kupata ushahidi kutoka vituo vyote 75.000 vya kupigia kura kwa kipindi cha siku mbili kutokana na ukubwa wa nchi. Ubalizi wa Marekani mjini Kinshasa umewatolea wito wagombea kutatua kwa amani na kwa mujibu wa sheria za Kongo migogoro ya uchaguzi.

Jumuiya ya Afrika Mashariki yampongeza Tshisekedi

Jumuiya ya nchi za Afrika Mashariki EAC yapongeza ushindi wa Felix Tshisekedi
Jumuiya ya nchi za Afrika Mashariki EAC yapongeza ushindi wa Felix TshisekediPicha: Philbert Rweyemamu/EAC

Tayari ujumbe wa pongezi kwa kwa Félix Tshisekedi umetolewa kutoka kwa baadhi ya wagombea uchaguzi akiwemo waziri mkuu wa zamani Adoplhe Muzito na wagombea wengine wadodo ambao walipata vchini ya asilimia moja za kura.

Kimataifa Marekani imesema imezingatia matokeo hayo yaliompa ushoindi rais Tshisekedi. Lakini hata hivyo, Ufaransa, Ubeljiji na nchi za Umoja wa Ulaya bado kutoa kauli yoyote kufuatia kutangazwa matokeo ya uchaguzi wa Kongo.

Kikanda viongozi kadhaa wamempongeza rais Tshisekedi kwa ushindi wake, ujumbe wa kwanza ulikuwa wa rais wa Burundi, Evariste Ndayishimiwe ukifuatiawa na ule wa Rais Samia Suluhu wa Tanzania.

Nchi zote za Afrika Mashariki pia zilipongeza ushindi wa Tshisekedi isipokuwa hasimu wake Rais Paul Kagame wa Rwanda. Nchi za jumuiya ya SADC pia zilimpongeza Tshisekedi.

Marais wengine ambao ukimya wao umeibua maswali mengi nchini Kongo ni pamoja na Denis Sassou Ngouesso wa nchi jirani ya Congo-Brazzabille, Joao Lourencou wa Angola na Faustin Arc-Ange Touadera wa Jamhuri ya Afrika ya Kati.