1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Utulivu wa mashaka warejea mpaka wa Gaza na Israel

Iddi Ssessanga
27 Machi 2019

Hali ya utulivu inaendelea katika ukanda wa Gaza kufuatia usitishaji mapigano usiyo rasmi kati ya Hamas na Israel, licha ya mashambulizi madogo kati ya pande hizo mbili. Israel imeendelea kuweka vifaru vyake mpakani.

https://p.dw.com/p/3Fkas
Palästina Israelischer Luftangriff auf den Gazastreifen
Picha: picture-alliance/ZumaPress/A.A. Alkahlout

Shule zimefungua tena kusini mwa Israel na wakaazi wakarejea shughuli zao za kila siku kufuatia mashambulizi ya usiku kati ya Israel na Hamas, na kuvunja utulivu uliokuwa umeshuhudiwa siku ya Jumanne, lakini hakukuwa na maafa yoyote ya binadamu kwa pande zote.

Kiongozi wa juu wa Hamas Ismail Haniye amejitokeza hadharani kwa mara ya kwanza tangu kuzuka tena kwa vurugu za sasa, na kutembelea vifusi vya iliyokuwa ofisi yake kabla ya kushambuliwa na Israel.

Haniye amesema Israel imepata ujumbe na kuwataka Wapalestina kujitokeza kwa wingi siku ya Jumamosi kushiriki maandamano ya kuadhimisha mwaka mmoja wa vuguvugu linalolenga kukomesha mzingiro wa Israel. Israel imeshaua zaidi ya Wapalestina 200 katika maandamano hayo.

Katika Ukingo wa Magharibi wakati huo, kijana wa Kipalestina mwenye umri wa miaka 18 alipigwa risasi na kuuawa wakati wa makabiliano kati ya wanajeshi wa Israel na waandamanaji. 

Luftangriff auf Gaza Stadt
Moto na moshi vikionekana wakati wa mashambulizi ya Israel mjini Gaza, Machi 25,2019.Picha: Reuters

Vita vya nne na Hamas?

Israel na Hamas wamepigana vita vitatu na makabiliano kadhaa tangu Hamas ilipochukuwa udhibiti wa ukanda wa Gaza mwaka 2007. Duru hii ya karibuni ya uhasama ilisababishwa na roketi lililofyatuliwa kutokea Gaza siku ya Jumatatu na kuangukia kwenye nyumba katikati mwa Israel na kuwajeruhi watu saba.

Msemaji wa Hamas Hazem Qassem, amesema vuguvugu hilo litaheshimu mpango wa usitishaji mapigano ikiwa Israel itafanya hivyo pia. "Ukanda wa Gaza umekuwa chini uvamizi wa Israeli kwa siku mili. Vuguvugu la Hamas lina haki ya kulinda watu wake wa Palestina," amesema Qassem.

"Hali imetulia baada ya uingiliaji wa ndugu zetu wa Misri na kutekeleza usitishaji mapigano. Hamas imedhamiria kuhakikisha utulivu maadam wakaliaji wanafanya hivyo pia wakati ikibakisha haki ya kuwalinda watu wa Palestina", amesisitiza.

Tangu mwaka 2015, Wapalestina wamewauwa Waisrael 50 katika matukio ya uchomaji visu, ufyatuaji risasi na mashambulizi ya kutumia magari katika Ukiongo wa Magharibi.

Na katika kipindi sawa, vikosi vya Israel vimeuwa zaidi wa Wapalestina 260. Israel inasema wengi wa Wapelestina waliouawa ni washambuliaji, lakini makabiliano kati ya waandamanaji na wanajeshi pia yamegeuka kuwa ya maafa.

Wakati uchaguzi wa Aprili 9 ukikaribia, waziri mkuu wa Israel anataka kuepusha madhara yasiotabirika ya kinachoweza kuwa vita vya nne na Hamas tangu mwaka 2008, lakini anakabiliwa na shinikizo kubwa la kisiasa.

rtre,ape,afptv.