1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uzoefu wa Uhispania katika kuzuwia uhamiaji haramu

Iddi Ssessanga
3 Machi 2017

Umoja wa Ulaya unajadili namna unavyoweza kupambana na uhamiaji haramu kutoka Afrika. Viongozi wa mataifa ya Ulaya wanakubaliana kwamba bila msaada wa mataifa wanakotokea wahamiaji, mapambano hayo hayawezakani.

https://p.dw.com/p/2YZog
Symbolbild Menschenhandel in der EU
Picha: picture alliance/dpa/PAO/Mittelmeer

Nahodha Antonio Queveso amesimama juu ya boti yake ya polisi katika bandari ya Dakar, macho yake yakielekezwa baharini. Taratibu inakarabia boti nyingine yenye urefu wa mita 30. Ni boti ya kikosi cha ulinzi wa kiraia cha Guardia. Ni polisi wa Uhisipania na Senegal katika doria ya pamoja ya mchana. Nahodha Quevedo anasema wanakagua kati ya boti nane hadi kumi kwa siku ambapo mbili kati ya hizo zinazuwiwa.

Polisi inahakiki ni watu gani waliomo kwenye boti hizo, na iwapo dani yake kuna wahamiaji waliofichwa. Quevedo anasema kwa sasa wanashughulika zaidi za boti za uvuvi na pale boti inaposhukuwa kutaka kusafiri kwenda kisiwani Canary, hurudishwa mara moja pwani.

"Ni kazi bure kwa sasa kujaribu njia ya majini. Mara moja moja tunawakamata watu wanaotoka mbali. Wanajaribu kwa muda wa miaka miwili kuja hapa Senegal au kwenda Mauritania kwa kutumia boti. Watu hawa huwekeza pesa nyingi na huishia kukamatwa nasi na kurejeshwa pwani," anasema Quevedo.

Flüchtlinge auf Boot im Mittelmeer
Boti iliowabeba wahamiaji haramu ikiwasili katika bandari ya Los Cristianos kwenye kisiwa cha Canary Julai 15 2006.Picha: picture-alliance/dpa

Ushirikiano na mataifa wanakotoka wahamiaji

Kiukweli ni kwamba hakuna Msenegali hata mmoja alieweza kufika canary katika miaka michache iliopita kwa kutumia boti. Njia hiyo imeimarishwa hasa baada ya wimbi la 2006 ambapo zaidi ya watu 30000 waliwasili katika kisiwa cha Canary. Serikali ya Uhispania iliingia makubaliano na Senegal, lengo likiwa kuwazuwia wahamiaji kutumia njia ya bahari kuelekea kisiwani hapo, na ikibidi wakamatwe hapo hapo baharini.

Alberto Virella alikuwa hadi muda mfupi uliopita akisimamia masuala ya Afrika katika wizara ya misaada ya maendeleo ya Uhispania. Hivi sasa ndiye balozi wa nchi yake nchini Senegal. "Siri ya mafanikio ya Uhisipania katika suala la uhamiaji ni ushirikiano na mataifa ya kanda katika njia tafauti," anasema balozi huyo wa Uhispania nchini Senegal.

Hii inamaanisha: Kupambana  dhidi ya umaskini, kukuza uchumi na kuimarisha uhusiano wa kibiashara na maingiliano ya kitamaduni. Ikiwa Umoja wa Ulaya unataka kudhibiti uhamiaji, unaweza kufanikiwa tu kwa kuyashirikisha mataifa wanakotokea wahamiaji hao. Na hata wafanyakazi wa ubalozi wa Umoja wa Ulaya mjini Dakar wanausifu mkakati huo wa Uhispania na kuupendekeza kama ruwaza kwa umoja huo.

Kama ilivyo kwa Ulaya hii leo, hata Uhispania ilikabiliwa na shinikizo kubwa huko nyuma. Mara nyingi bahari hiyo ilitema maiti za Waafrika kwenye ufukwe wake wa mapumziko. Uhispania illitikia kwa kuipatia Senegal kiasi cha euro milioni 20, ambazo pamoja na mambo mengine, zilitumika kuimarisha operesheni za jeshi la polisi katika mapambano dhidi ya uhamiaji haramu. Kamishna Mamadou Ndiaye Fall, anahusika na uhamiaji haramu katika polisi ya Senegal.

Mittelmeer Flüchtlinge auf Lampedusa
Wahamiaji wa Kiafrika wakiwa kisiwani Lampedusa baada ya kuokelewa kwenye boti katika bahari ya Mediterrania.Picha: DW/D. Cupolo

"Uhispania iliipatia senegal uwezo wa kiufundi ili kuweza kuendesha iperesheni. Tunazo boti bandarini, ambazo zinafanya doria mara kwa mara. Tuna helikopta ya kijeshi inayoruka juu ya bahari na kuzifuatilia boti  za wahamiaji. Na hapa katika polisi ya mpakani tunacho kitengo kilichowezeshwa vizuri kuchunguza mitandao ya wasafirishaji haramu wa watu," anasema Kamishna Ndiaye.

Nani awajibike zaidi?

Pamoja na yote hayo, Wasengali bado ni miongoni mwa makundi makubwa zaidi ya wahamiaji wanaokwenda Ulaya kupitia bahari ya Mediterrania. Miaka 10 tangu kuanza kwa makubaliano kati ya Senegal na Uhispania, Wasenegal wengi bado hawataki kubakia nyumbani. Je, nchi hiyo haiwezi kulinda mipaka yake bila msaada kutoka Uhispania? Afisa wa polisi Antonio Quevedo ana maoni haya.

"Uhamiaji ni tatizo letu. Wasenegali wanatusaidia tu, lakini tatizo la uhamiaji ni la Uhispania na Ulaya. Ikiwa tutajitoa hapa siuji inaweza kuchukuwa muda gani kabla hawajaanza tena safari. Serikali ya Senegal haiwezi kujua ni lini watu watafanza safari. Ni jambo la kimantiki,'' anasema Nahodha Antonio Quevedo katika maoni yake binafsi.

Mwandishi: Marc Dugge

Tafsiri: Iddi Ssessanga

Mhariri: Daniel Gakuba