1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vigogo uwanjani Ligi ya Mabingwa Ulaya

Admin.WagnerD15 Septemba 2015

Hatimae ule wakati umewadia kwa vigogo vya soka barani Ulaya kufunguwa dimba katika michuano ya ligi ya mabingwa katika awamu ya makundi ambapo timu 16 ziko uwanjani Jumanne (15.09.2015) katika mechi nane.

https://p.dw.com/p/1GWyv
Wachezaji wa Wolfsburg Julian Draxler (kulia) na Josuha Guilavogui.
Wachezaji wa Wolfsburg Julian Draxler (kulia) na Josuha Guilavogui.Picha: picture-alliance/dpa/P. Steffen

Ujerumani inawakilishwa na timu mbili katika michuano hiyo Wolfsburg na Borussia Monchengladbach timu hizo zimekuwa zikisubiri kwa hamu michuano hiyo ya vigogo vya usoka barani Ulaya na timu zote mbili zitakabiliana na timu ambazo inazifahamu vyema.

Kwa Wolfsburg miaka sita ya kuwa nje ya michuano hiyo ni mingi sawa na kama vile miaka sitini.Historia kujirudia tena leo wakati timu hiyo itakapochuana na CSKA Moscow ya Urusi ni suala lilioko mdomoni.Mchuano wa mwisho timu hiyo iliichabanga CSKA Moscow mabao 3-1.

Mafanikio ya mwaka 2008- 2009 yalioshuhudia Mbwamwitu hao wa Ujerumani kwa kutwaa ubingwa wa Ujerumani kwa mara ya kwanza kabisa na pia baadae kujipatia nafasi ya kufuzu kwenye michuano ya ligi ya mabingwa barani Ulaya,timu hiyo ikijilinganisha na mwaka 2009 inajiona iko imara zaidi kama timu.

Yarudi tena baada ya miaka 37

Kwa upande wa wawakilishi wengine wa Ujerumani katika michuano hiyo Borussia Monchegldabach kusema kwamba msimu wao wa soka umedorora kutokana na kuendelea kupwaya hadi sasa itakuwa ni kuikadiria vibaya.

Wachezaji wa Borussia Mönchengladbach wakiwa katika mazoezi.
Wachezaji wa Borussia Mönchengladbach wakiwa katika mazoezi.Picha: Getty Images/AFP/C. Quicler

Inaingia uwanjani leo hii kumenyana na mabingwa wa ligi ya Ulaya Sevila ya Uhispania timu ambayo imewahi kuchuana nayo katika pambano jengine la Ulaya ikiwa ni miezi saba tu iliopita. Kurudi kwa timu hiyo katika ligi ya mabingwa baada ya miaka 37 kumekuwa sio kwa shangwe hasa baada ya kupoteza michezo minne mfulululizo katika ligi ya Ujerumani.

Paris St.Germain vigogo vinavyolidhibiti kabumbu la Ufaransa vinajimwaga kuonyesha umahiri wao dhidi ya Malmo ya Sweden.ambao ni washindi wa pili wa michuano ya Kombe la Ulaya mwaka 1979 na ni mara ya pili kushiriki ligi ya mabingwa kufuatia mara yao ya kwanza mwaka jana.

Kivumbi chaikabili Real Madrid na Manu

Real Madrid nayo inakabiliwa na kajivumbi itakapokutana na wazoefu wa michuano hii ya ligi ya mabingwa Shakhtar Donetsk ya Ukraine. Christiano Ronaldo amezima hofu yoyote ile juu ya uzima wake kwa mtindo wa aina yake ambapo aliifungia timu yake hiyo ya Real Madrid mabao 5 kati ya 6-1 dhidi ya Espanyol katika ligi ya Uhispania ya La Liga.

Cristiano Ronaldo bado wamo.
Cristiano Ronaldo bado wamo.Picha: Reuters/A. Gea

Manchester United ya Uingereza imerudi tena katika ligi ya mabingwa baada ya kutimuliwa msimu uliopita leo wao wanachuana na PSV Eindhoven huko Uholanzi. Nahodha wa Manu Wayne Rooney atakasokena katika mpambano wa leo kutokana jeraha lakini macho ya mashabiki wa timu zote mbili yatamkodolea Memphis Dopey aliyenunuliwa na Manu kutoka timu ya PSV.

Mabingwa wa Uturuki Galatasaray walikuwa na muda wao wa kuchekelea katika kabumbu la Ulaya hapo mwaka 2000 wakati ilipoitowa Arsenal kwa mikwaju ya penelti na kushinda Kombe la UEFA kama lilivyokuwa likijulikana wakati huo.Leo hii inawakaribisha Atletico Madrid liofikia fainali ya michuano hiyo mwaka 2014 na na mara ya mwisho kulitwaa kombe la Ulaya ikiwa ni mwaka 1962.

Vigogo wengine vilioko uwanjani leo hii ni vile vya Ureno Benfica ambao chuchupu waliukosa ubingwa wa Ulaya tokea mwaka 1961 na mwaka 1962 na pia wakati walipopoteza katika fainali kwa Chelsea hapo mwaka 2013 na kwa Sevilla hapo mwaka 2014.Leo wanakwaruzana na wanagennzi wa michuano huu Astana wa Kazakstan.

Mpambano mwengine wa leo ni kati ya Machester City na Juventus kwa timu hizo wakati utawasemea.

Mwandishi : Mohamed Dahman/AFP

Mhariri :