1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaYemen

Wahouthi wazidisha mashambulizi katika Bahari ya Shamu

Tatu Karema
27 Januari 2024

Waasi wa Houthi wa Yemen jana walizidisha mashambulizi dhidi ya meli zinazotumia Bahari ya Shamu na kushambulia meli ya mafuta kwa jina Marlin Luanda inayoendeshwa kwa niaba ya kampuni ya kibiashara ya Trafigura

https://p.dw.com/p/4bjmM
Meli ya Galaxy leader iliyotekwa na waasi wa Houthi katika Bahari ya Shamu mnamo Novemba 22,2023
Meli ya Galaxy leader safarini kupitia Bahari ya ShamuPicha: Houthi Media Centre/AFP

Kampuni ya kibiashara ya Trafigura imesema kuwa meli hiyo ya mafuta ililengwa na kombora ilipokuwa ikipita katika Bahari hiyo ya Shamu. Taarifa iliyotumwa na kampuni hiyo kwa njia ya barua pepee, imesema vifaa vya kuzima moto kwenye meli hiyo vinatumiwa kuzima na kudhibiti moto huo.

Soma pia:Uingereza na nchi washirika washambulia maeneo ya Kihouthi Yemen

Mapema Ijumaa, shirika linalosimamia operesheni za biashara kupitia kwenye bahari nchini Uingereza (UKMTO) na Kampuni ya usalama ya baharini ya Uingereza Ambrey, zilisema kuwa zilipokea taarifa za meli kulengwa katika Bahari ya Shamu karibu na Ghuba ya Aden ya Yemen na moto kuzuka ndani ya meli hiyo.

Houthi yathibitisha kuhusika na shambulizi

Msemaji wa tawi la kijeshi la kundi hilo la Houthi, amethibitisha kuwa vikosi vya baharini vilifanya operesheni iliyolenga meli hiyo ya 'Uingereza' katika Ghuba ya Aden na kusababisha kuzuka kwa moto huo.