1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahouthi watuhumiwa kuvunja makubaliano

Josephat Charo
6 Machi 2019

Serikali ya Yemen na washirika wake Saudi na Emirates zimewatuhumu waasi wa kihouthi kutozingatia makubaliano yao ya kuondoa vikosi kutoka eneo la bahari ya Shamu.

https://p.dw.com/p/3EYZq
Jemen Hafenstadt Hudaida ARCHIV
Picha: picture-alliance/dpa/H. Al-Ansi

Waasi wa kihuthi walikubali kuondoa vikosi katika maeneo ya bandari ya Saleef na Ras Issa vilivyokuwa vikiyashikilia baaada ya mazungumzo ya mwezi uliopita ikiwa ni hatua muhimu katika kumaliza vita  ambavyo vimedumu kwa karibu miaka minne.

Kwa mujibu wa barua  iliyoandikwa kwa Katibu mkuu wa umoja wa Mataifa Antonio Guterres, Serikali ya Yemen, Saudi Arabia na Umoja wa Falme za Kiarabu zimeliomba baraza za usalama kuwataka wahuthi kusitisha shughuli zao katika eneo la bahari ya shamu lenye mtafaruku.

Tangu makubaliano ya awali ya kuweka silaha chini yaliofanyika nchini Sweden  mwezi Desember, Saudi , washirika wa Yemen na wa Huthi wamekuwa wakituhumiana kukiuka makubaliano lakini Umoja wa mataifa umekuwa ukiepuka kulaumu upande wowote.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa Stephane Dujaric amesema majadiliano yanaendelea kati ya pande mbili ili ziweze kutimiza ahadi na kuondoa vikosi katika eneo la bandari. Baraza la usalama linatarajiwa kuijadili Yemen Machi 19 licha ya wasiwasi kuwa huenda makubaliano kati ya pande hizo mbili yakavunjika.

UN Sprecher Stephane Dujarric ARCHIV 2018
Stephane Dujarric, msemaji wa Umoja wa MataifaPicha: picture-alliance/Photoshot/L. Muzi

Umoja wa mataifa umesema unatumaini kwamba utulivu katika eneo la Hodeida utaruhusu msaada wa haraka wa dawa na chakula kuwafikia mamilioni ya watu wenye uhitaji nchini Yemen.

Akizungumzia hali ilivyo hivi sasa na kuhusu matumaini ya majadiliano na hali ya utoaji misaada ya chakula katika eneo la mgogoro msemaji wa Shirika la chakula duniani Herve Verhoosel alisema, "Namaanisha  pande zote zinafanya mazungumzo. Wanazungumzia kuondoa majeshi katika eneo husika. Yote haya yanakuja kwa pamoja. Tunatumaini pande zote zitaendeleza mazungumzo na tutaweza kuona matokeo ya mjadala. Kufika eneo hilo ni muhimu na ni wakati sasa wa kuwapa raia kipaumbele.'' 

Hodeida ni eneo linalotumika kuingiza bidhaa na misaada nchini Yemen, inayotajwa na Umoja wa Mataifa kuwa nchi yenye mgogogro mbaya zaidi wa kibinaadamu kuwahi kutokea.

Muungano unaoongozwa na Saudi Arabia umeainisha visa visa 1754 vya ukiukaji, tangu kuanya kutekelezwa kwa makubaliano ya kusitisha mapigano Desemba 18 na kwamba zaidi ya askari 125  wa vikosi vinavyoiunga mkono serikali waliuawa.

(AFPE)