1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waasi wa Yemen waushambulia mpaka wa Saudia

1 Mei 2015

Saudi Arabia imesema majeshi yake yamewauwa na waasi wa Yemen waliofanya shambulizi lao la kwanza kubwa dhidi ya nchi hiyo tangu kuanza mwezi uliopita mashambulizi ya angani yanayoongozwa na Saudia

https://p.dw.com/p/1FIfB
Saudi Arabien Jemen Krise Soldat an der Grenze
Picha: Reuters/F. Al Nasser

Wizara ya ulinzi ya Saudi Arabia imesema wanajeshi wake watatu pia waliuawa katika mapambano hayo baada ya waasi wa Houthi kuvilenga vituo vyao vya uangalizi, wakati jeshi lake likijaribu kuzuia shambulizi hilo.

Kumekuwa na makabiliano hapo kabla lakini hii ni mara ya kwanza ambapo jeshi la Saudi Arabia limeripoti kuhusu shambulizi kamili la waasi wa Houthi katika mipaka yake. Katika mji mkuu Sanaa, mashambulizi mapya ya kutokea angani yanayoongozwa na Saudia yamefanywa katika uwanja wa ndege ikiwa ni siku chache tu baada ya ndege za kivita kuilipua njia ya ndege katika uwanja huo ili kuzuia ndege moja ya Iran kutua.

Wakati huo huo, mawaziri wa mataifa ya Ghuba hapo jana walipinga pendekezo la kuandaa mazungumzo katika nchi isiyounga mkono upande wowote katika mzozo wa kisiasa nchini Yemen, wakati ripoti ya watalaamu ikisema kuwa Iran imekuwa ikiwapa silaha waasi wa Houthi tangu mwaka wa 2009.

Jemen Luftangriff auf dem Flughafen in Sanaa
Ndege za kivita zinazoongozwa na Saudi Arabia zimeushambulia tena uwanja wa ndjege wa YemenPicha: Reuters/K. Abdullah

Umoja wa Mataifa unajaribu kumaliza operesheni ya angani iliyodumu wiki kadhaa, na kuzirejesha pande zote mbili katika meza ya mazungumzo. Baada ya mkutano wa mjini Riyadh, mawaziri wa nchi za Ghuba walisisitiza kuwa mazungumzo baina ya makundi hasimu ya kisiasa nchini Yemen yaandaliwe nchini Saudi Arabia, ambayo inaongoza muungano wan chi za Kiarabu dhidi ya waasi wa Kishia tangu Machi.

Iran inapendekeza kuandaa mazungumzo ya Umoja wa Mataifa ili kumaliza vita nchini Yemen katika taifa lisiloegemea upande wowote, ambalo haliwakilishwi katika muungano unaoongozwa na Saudia.

Baraza la Ushirikiano wa Ghuba lenye nchi sita wanachama limesisitiza kuunga mkono juhudi kali zinazofanywa na serikali halali ya Yemen za kuandaa mkutano chini ya mwamvuli wa Baraza hilo mjini Riyadh.

Katibu Mkuu wa Baraza hilo Abdullatif al-Zyani amesema mkutano huo utahudhuriwa na “pande zote za Yemen na zinazounga mkono uhalali na usalama na uimara wa Yemen”.

Mkutano wa jana wa nchi za Ghuba ambazo ni Bahrain, Kuwait, Oman, Qatar na Umoja wa Falme za Kiarabu, ulilenga kuweka msingi wa mkutano mkuu wa viongozi wa Baraza hilo utakaoandaliwa Jumanne wiki ijayo, na ambao pia utahudhuriwa na Rais wa Ufaransa Francois Hollande.

Mgogoro huo umeongeza mivutano katika kanda hilo. Iran inayotuhumiwa kwa kuwapa silaha waasi wa Houthi, imesema meli zake mbili zilizotumwa katika Ghuba ya Aden zimefika mlango wa Bab al-Mandab, njia muhimu ya bahari baina ya Yemen na Djibouti. Iran inasisitiza kuwa meli zake hizo hazitafika katika mipaka ya bahari ya nchi nyingine.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP
Mhariri: Gakuba Daniel