1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wapiganaji wa Al Shabaab waapa kufanya mashambulio zaidi.

Halima Nyanza15 Julai 2010

Kundi la waasi wa al-Shabaab nchini Somalia, linalodaiwa kuwa na mafungamano na mtandao wa kigaidi wa al Qaeda limeapa kufanya mashambulio zaidi, baada ya kukiri kuhusika na shambulio lililotokea nchini Uganda.

https://p.dw.com/p/OLXE
Wapiganaji wa al Shabaab ambo wameapa kufanya mashabulio zaidi.Picha: AP

Kiongozi wa kundi hilo la al Shabaab Mohamed Abdi Godane ambaye pia anajulikana kama Abu Zubairy alisema katika ujumbe uliotangazwa na radio za nchi hiyo, kwamba shambulio hilo la kampala ni mwanzo tu, na kuongeza kuwa watalipiza kisasi dhidi ya mashambulio yaliyofanywa na kikosi cha Jeshi la Kulinda amani cha Umoja wa Afrika -AMISOM nchini Somalia na kusababisha vifo vya raia.

Kundi hilo tayari limekiri kwamba shambulio hilo ni kulipiza kisasi ya kuwepo kwa kikosi cha Uganda katika kikosi hicho cha AMISOM, nchini Somalia.

Al shabaab mara kwa mara limekuwa likitishia kufanya mashambulio katika eneo hilo la Afrika, lakini shambulio la Uganda ni la kwanza kufanywa nje ya Siomalia.

Aidha amesema kuwa shambulio hilo la Kampala limefanywa na kikosi cha wapiganaji hao wa al Shabaab cha Saleh Nabhan, baada ya mtuhumiwa katika shambulio lililotokea Mombasa mwaka 2002 dhidi ya Israel, ambaye ni mwanachama wa al Qaeda mwenye asili ya Kenya, kuuawa katika shambulio la anga lililofanywa na marekani mwaka uliopita.

Wakati al Shabaab wakiapa kuendelea kufanya mashambulio, Uganda imesema inaweza kupeleka tena kikosi cha wanajeshi 2,000 wanaohitajika, katika kikosi cha Umoja wa Mataifa cha kulinda amani nchini Somalia.

Msemaji wa jeshi la Uganda Felix Kulayigye amesema nchi yake inaweeza ikachangia wanajeshi hao ama zaidi katika jeshi hilo la Umoja wa Afrika iwapo nchi nyingine zitashindwa kufanya hivyo.

Akizungumzi jana kuhusiana na kikosi hico Rais Museveni alisema IGAD itaongeza wanajeshi.

Wakati mkutano wa Umoja wa Afrika ukitarajiwa kufanyika wiki ijayo nchini Uganda, mataifa wanachama wa umoja huo yameelezwa kushindwa kutimiza ahadi zao za kuchangia wanajeshi katika kikosi hicho.

Kikiwa na wanajeshi wachacche zaidi ya elfu saba, kikosi hicho cha AMISOM kimeweza kwa kiasi kuwepo mpaka sasa kwa serikali ya mpito unayoungwa mkono na nchi za magharibi ambayo inaoongozwa na Rais Sharif Sheikh Ahmed, lakini jeshi hilo limeshindwa kuwamaliza nguvu wapiganaji nchini humo.

Katika hotuba yake jana Rais Musseveni  alizitaka nchi za Afrika kupeleka wanajeshi wake katika jeshi hilo ili kuliongeza na kufikia kikosi cha wanajeshi elfu 20, na kwamba kwa kushirikiana na serikali hiyo ya mpito ya Somalia kuweza kuwamaliza magaidi nchini humo.

Wakati huohuo wachunguzi wa Uganda kuhusiana na shambulio la kigaidi lililotokea mwishoni mwa wiki iliyopta, bado wanaendelea kuchunguza mazingira ya shambulio hilo la mjini Kampala na kuwatambua watu waliouawa..

Mwandishi: Halima Nyanza(afp)

Mhariri:  Abdul-Rahman