1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Watetezi wa demokrasia Myamnar wageukia bunduki

John Juma
7 Februari 2024

Waandamanaji wamekabiliana tena na jeshi nchini Myanmar, lakini sasa si kwa mabango tu, bali kwa kufyatuliana nao risasi - ishara kwamba watetezi hao wa demokrasia wamekuja na mbinu mpya za kukabiliana na wanajeshi.

https://p.dw.com/p/4c8Mc
Wanajeshi wa Myanmar wakiwa kwenye doria kufuatia maandamano ya watetezi wa demokrasia.
Wanajeshi wa Myanmar wakiwa kwenye doria kufuatia maandamano ya watetezi wa demokrasia.Picha: AFP/Getty Images

Miaka mitatu iliyopita, waandamanaji vijana nchini Myanmar waliokuwa wakibeba mabango yenye jumbe mbalimbali kutetea demokrasia ya taifa lao baada ya mapinduzi ya kijeshi, walitawanywa na wanajeshi katika mitaa ya Mandalay.

Lakini mwezi Januari 2024, hali ilikuwa tofauti katika maandamano yaliyofanyika jimbo la kaskazini Shah, kwani waandamanaji hao walionekana wakifyatua risasi kwa ustadi dhidi ya wanajeshi.

Soma zaidi: Utawala wa kijeshi Myanmar wanyonga wanaharakati wanne

Mapinduzi yaliyofanyika miaka mitatu iliyopita yalipaswa kurudisha udhibiti wa Myanmar mikononi mwa wanajeshi baada ya majaribio ya miaka 10 ya utawala wa kidemokrasia.

Badala yake, yaliitumbukiza nchi kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe, yakaharibu uchumi na ikawachochea maelfu ya vijana kujiunga na kile waanachokiita kuwa “Vikosi Vya Ulinzi vya Wananchi (PDF)” na kupigania demokrasia yao kwa kutumia bunduki.

Myanmar Aung San Suu Kyi
Muandamaji akiwa amebeba picha ya kiongozi wa Myanmar aliyepinduliwa, Aung San Suu Kyi.Picha: JACK TAYLOR/AFP/Getty Images

Vikosi vya PDF vinajumuisha vikundi vidogo vidogo katika maeneo muhimu ya Myanmar hadi katika maeneo ya mpakani, ambako vikundi vya waasi wa kikabila vilivyoimarika zaidi vina udhibiti.

Vifo zaidi, hasira zaidi

Ni vigumu kubaini ni watu wangapi wameuawa kwenye machafuko nchini humo, lakini kulingana na shirika linalofuatilia haki za binadamu, watu wasiopungua 4,400 wameuawa kutokana na ukandamizaji wa wanajeshi dhidi ya wakosoaji wake. 

Jeshi linasema wapinzani wake ndio waliowaua zaidi ya raia 6,000 hadi sasa na linawataja wapiganaji wa PDF kuwa magaidi wanaolenga kuivunja nchi.

 Myanmar | National League for Democracy (NLD)
Muandamanaji akiwa na bendera ya chama cha NLD cha kiongozi aliyepinduliwa nchini Myanmar, Aung Saan Suu Kyi.Picha: Peerapon Boonyakia/picture alliance/ZUMAPRESS/SOPA Images

"Miaka kadhaa ya mashambulizi kutoka kwa jeshi linalotumia silaha za Urusi na China imewafanya wapiganaji wengi wa PDF kuwa vikosi imara vya kivita," alisema Sugar, mmoja wa makamando wa vikosi hivyo.

Soma zaidi: Aung San Suu Kyis kutoka katika kifungo cha nyumbani

"Uzoefu wetu katia uwanja wa vita umetufanya kuwa askari tofauti. Tunajifunza kupigana na tunapigana tukiendelea kujifunza. Tunajua zaidi kuhusu wanajeshi na pia tuna mawasiliano bora kati ya askari wetu wa PDF. Hatuhitaji kuzungumza na kila mmoja katika vita. Tunatumia ishara za mikono pekee. Sisi ni bora zaidi."

Myanmar | Maandamano
Polisi wa Mnyanmar wakiwatia watu nguvuni mjini Yangon kufuatia maandamano dhidi ya utawala wa kijeshi.Picha: Ye Aung Thu/AFP/Getty Images

Kauli kama hiyo pia ilitolewa na Ko Phyo ambaye zamani alikuwa mwalimu lakini sasa ni mpiganaji katika PDF. "Tunao uwezo wa kumshinda kila mwanajeshi katika ngome yake," aliongeza.

Kwa Ko Phyo na wataalamu wengine - wakiwemo masoroveya, walimu na wanafunzi - wanaamini mapinduzi ya hivi punde yalikuwa uthibitisho kwamba mapambano yasiyo ya vurugu ya demokrasia yaliyoongozwa kwa miongo kadhaa na mshindi wa Tuzo ya Nobel, Aung San Suu Kyi, kamwe hayangewaondoa wanajeshi madarakani.

Hata kama wengi hawaamini kwamba vikundi vya PDF vinaweza kuliangusha jeshi ambalo limeiongoza Myanmar kwa kipindi cha miaka 70 ya uhuru wa nchi hiyo, lakini miungano yao mbalimbali na makundi ya kikabila yenye silaha, ambayo baadhi yao yamepigana dhidi ya wanajeshi kwa miongo kadhaa, bila shaka yanautikisa utawala huo.

Chanzo: AFPE