1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri Mkuu wa Uingereza yuko Pakistan baada ya kuizuru India

Mohamed Dahman14 Desemba 2008

Waziri Mkuu wa Uingereza Gordon Brown amelilaumu kundi la wanamgambo lenye makao yake nchini Pakistan Lashkar- e- Taiba kwa mashambulizi yaliosababisha maafa makubwa dhidi ya mji wa Mumbai nchini India mwezi uliopita.

https://p.dw.com/p/GFp0
Waziri Mkuu wa Uingereza Gordon Brown(kushoto) akiwa na Waziri Mkuu wa India Manmohan Singh katika ziara fupi mjini New Delhi, India, leo hii tarehe 14 December 2008 kabla ya kuelekea Pakistan.Picha: picture-alliance / dpa

Kauli yake hiyo inakuja wakati wakati hali ya mvutano kati ya India na Pakistan ikitokota leo hii.

Pakistan imesema hapo jana ndege za kivita za India zimekiuka naga yake lakini serikali ya India baadae imekanusha tukio hilo na kuituhumu Pakistan kwa kujaribu kufanya ubabaishaji.

Waziri Mkuu wa Uingereza leo alikutana na Waziri Mkuu wa India Manmohan Singh wakati wa ziara fupi katika mji mkuu wa India New Delhi na kusema kwamba atafikisha suala la mashaka ya India kuhusiana na mashambulizi ya Mumbai kwa Rais Asif Ali Zardari wa Pakistan leo hii.

India ikiungwa mkono na Marekani imeitaka Pakistan kuyavunja makundi ya wanamgambo wa itikadi kali za Kiislam yalioko nchini Pakistan kufuatia mashambulizi ya mji wa Mumbai yaliouwa watu 179 mwezi uliopita.

Imelilaumu kundi la Lashkar-e-Taiba kwa mashambulizi hayo ambalo imesema limeundwa na Pakistan kupambana na utawala wa India katika jimbo la Kashmir linalogombaniwa na nchi hizo mbili.