1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri wa spoti wa Togo auwawa ajali ya ndege

Ramadhan Ali4 Juni 2007

Misiba 2 mikuu imegubika changamoto za mwishoni mwa wiki za Kombe la Afrika la Mataifa mjini Freetown na Lusaka.Nchini zambia vurumai uwanjani imesababisha vifo 12 wakati huko Sierra Leone,helikopta iliompakia waziri wa michezo ilipatwa na ajali.

https://p.dw.com/p/CHc3
Mohammed Zidane-stadi wa mabingwa wa Afrika:Misri.
Mohammed Zidane-stadi wa mabingwa wa Afrika:Misri.Picha: picture alliance / dpa

Katika kinyan’ganyiro cha Kombe la Afrika la mataifa-Ugandan Cranes-timu ya Taifa ya Uganda imenguruma mbele ya Super Eagles-Nigeria mjini Kampala.

Taifa Stars –Tanzania na Harambee Stars-Kenya, zimemudu suluhu tu mbele yas Senegal na Swaziland huko Mwanza na Mbabane.Kinyan’ganyiro hicho cha kuania tiketi za kombe la Afrika nchini Ghana 2008,kimegubikwa na misiba 2 mikubwa:

Mjini Freetown-waziri wa michezo wa Togo na watu wengine 20 wameuwawa katika ajali ya ndege wakati ikitua katika uwanja wa ndege wa Sierra Leone kwa changamoto ya kombe la Afrika.Na mjini Lusaka, si chini ya mashabiki 12 wameuwawa baada ya vurumai na mkanyagano wakati wakiharakisha kutoka uwanjani baada ya Zambia kuwazaba simba wa J.K.Kongo mabao 3:0.

Ujerumani pia ilikuwa uwanjani jumamosi kwa kinyan’ganyiro cha kuania tiketi za finali ya ya kombe la Ulaya la mataifa hapo mwakani:Ujerumani iliizaba San Marino mabao 6-0-lakini haikupata mteremko wa duru ya kwanza walipoicharaza San Marino nyumbani mwao mabao 13-0.

Swali jumamosi halikuwa ushindi wa Ujerumani,bali kwanini-mshambulizi wao hatari Miroslav Klose hakutia bao na kwanini mkuki wake umeingia kutu ?

Ni wiki kadhaa tangu katika Bundesliga anakoichezea Werder Bremen,Klose hakutikisa wavu:

Kocha wa Ujerumani Joachim Loew,hata hivyo ana imani na Klose na anapanga kumteremsha tena uwanjani jumatano hii ijayo pale Ujerumani itakapopambana na Slovakia kuania tiketi ya kombe la Ulaya.

Akielezea kumuelewa kwake Klose na hali yake ya sasa, kocha wa Ujerumani Loew alisema:

“Nadhani kila mshambulizi ana kipindi chake cha msukosuko.Hivi sasa Miroslav klose hayupo katika hali nzuri,lakini uhodari wake hauna shaka.Yafaa kumsaidia kujikomboa kutoka hali yake ya hivi sasa.”

Kocha mwengine wa taifa wa Ujerumani ingawa wa zamani Berti vogts alikiona jumamosi kile kilichomtoa kanga manyoya mjini Kampala.Kwani,Ugandan Cranes-timu ya taifa ya Uganda haikumjali Berti Vogts wala Nwanko Kanu walioilaza Nigeria kwa mabao 2:1.

Timu nyengine ya Afrika mashariki iliotamba nyumbani ni taifa Stars-Tanzania ingawa ilitoka suluhu- bao 1:1 na Senegal huko Mwanza.

Harambee Stars ilimudu suluhu mjini Mbabane na matarajio yake ya kusonga mbele yamefifiabaada ya Kenya kumudu suluhu mjini Mbabane na Swaziland .

Kinyan’ganyiro cha Kombe la Afrika mwishoni mwa wiki kimezusha misiba 2 mikubwa:wa kwanza ni ule wa ndege iliompakia waziri wa spoti wa Togo na abiria wengine 20 kwenda Freetown kuangalia mpambano na Liberia uliomalizika kwa ushindi wa Togo wa bao 1:0.

Waziri wa spoti wa togo Atipe Kwako alikuwa miongoni mwa raia 18 wa kitogo ndani ya helikopta ilioshika moto wakati ikijaribu kutua na kujigonga uwanjani ndege.Mmoja kati ya watumishi wa ndege hiyo wa kirusi alinusurika na maisha.Jumla ya watu 22 walikuwa ndani ya helikopta hiyo.

Wakati Togo ikiomboleza kifo cha waziri wake wa michezo na raia wake wengine ,rais Levy Mwanawasa wa Zambia ameamrisha jana uchunguzi kujua chanzo cha vurumai na mkanyagano uliozuka uwanjani hadi mashabiki 12 kupoteza maisha na darzeni kujeruhiwa baada ya Zambia kuilaza J.K.Kongo mabao 3:0 huko Chililabomwe ,ukanda wa shaba.mashabiki 5 zaidi walifikishwa hospitali.

Kwa jumla, simba wa nyika Kamerun,Tembo wa Ivory Coast na simba wa Atlas wa Morocco, wanahitaji pointi 1 tu sasa kwenda Accra, mwakani kwa kombe la Afrika.