1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Xi awasili Myanamar kwa ziara ya kihistoria

Yusra Buwayhid
17 Januari 2020

Xi atasaini miradi kadhaa ya miundombinu kama sehemu ya mpango wa biashara ya kimataifa wenye lengo la kupanua ushawishi wa China katika eneo la Asia. Lakini ziara ya Xi imezua hofu miongoni mwa wanaharakati.

https://p.dw.com/p/3WN9g
Mynmar | Xi Jinping auf Staatsbesuch
Picha: picture ´-alliance/AP Photo/A. Shine Oo

Rais Xi Jinping wa China aliwasili Myanmar siku ya Ijumaa (Januari 17) kwa ziara rasmi ya siku mbili yenye lengo la kuadhimisha miaka 70 ya uhusiano wa China na Myanmar pamoja na kuiunga mkono serikali ya Aung San Suu Kyi inayokabiliwa na ukosoaji wa kimataifa.

Siku moja kabla ya kuwasili, gazeti linalomilikiwa na serikali ya Myanmar la New Light lilimnukuu kiongozi huyo wa China akitoa wito wa maendeleo wa miradi tofauti ya miundombinu ya China, ikiwa ni pamoja na ule wenye utata wa ujenzi wa bandari wenye thamani ya dola za Kimarekani bilioni 1.3 unaojengwa katika jimbo la Rakhine lilokumbwa na vurugu.

Bandari hiyo itafungua njia mpya ya biashara ambayo itaiunganisha China na mji wa Kyaukphyu wa jimbo la Myanmar la Rakhine kupitia Bahari ya Hindi. Mradi mwengine unaotarajiwa kati ya mataifa hayo mawili ni ujenzi wa njia ya reli ya mwendo kasi.

"Ziara hii ya kihistoria pia itazaa matunda ya kihistoria," alisema naibu waziri wa mambo ya nje wa China, Luo Zhaohui, akiwa katika mkutano na waandishi habari wiki iliyopita.

Mynmar | Xi Jinping mit Aung San Suu Kyi
Rais wa China Xi Jinping akiwa na kiongozi wa Myanmar Aung San Suu KyiPicha: picture-alliance/AP Photo/A. Shine Oo

Xi alitarajiwa kukutana na Rais wa Myanmar Win Myint na waziri wa mambo ya kigeni na kiongozi asiye rasmi wa taifa hilo, Aung San Suu Kyi, katika sherehe ya kumkaribisha kwenye mji mkuu wa Naypyitaw ikifuatiwa na mkutano na mkuu wa majeshi, Min Aung Hlaing, siku ya Jumamosi.

Xi awakasirisha wanaharakati

Wanaharakati walitarajiwa kuandamana katika mji wa biashara wa Yangon siku ya Jumamosi dhidi ya mradi wa China.

Rakhine ni jimbo maskini zaidi nchini Myanmar na limeshuhudia machafuko makubwa pamoja na mauaji. Zaidi ya watu 700, 000, wengi wao wa jamii ya Rohingya, wamekimbilia nchi jirani ya Bangladesh kutokana na vurugu hiyzo, huku maelfu wakiwa wamepoteza makazi yao.

China inaitetea na kuinga mkono Myanmar katika Umoja wa Mataifa, ambako shinikizo la kimataifa linazidi kuongezeka kasi kudai uwajibikaji juu ya mgororo huo unaowahusu watu wa jamii ya Rohingya.

Ziara ya Xi imezua hofu miongoni mwa wanaharakati wanaopigania haki za binadamu wanaosema kwamba miradi ya China itasababisha upokonyaji wa ardhi pamoja na kuharibu mazingira, mchambuzi David Mathieson ameliambia shirika la habari la Ujerumani la dpa.

Hata hivyo, kwa baadhi, China ni muokozi wa kiuchumi kwa Myanmar.

Biashara kati ya nchi hizo mbili ilikuwa na thamani ya dola za Marekani bilioni 16.8 mwaka 2019 na sehemu kubwa ya deni la kigeni la Myanmar la asilimia 40 limekopeshwa na China.

Vyanzo: (AFP, Reuters, dpa)