1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMarekani

Xi: Uhusiano wa Marekani na China ni muhimu kwa dunia

9 Oktoba 2023

Rais wa China Xi Jinping amesema uhusiano kati ya nchi yake na Marekani utaathiri mustakabali wa binadamu, wakati akikutana na kundi la maseneta wa Marekani mjini Beijing.

https://p.dw.com/p/4XJmw
Rais wa China Xi Jinping na mwenzake wa Marekani Joe Biden
Rais wa China Xi Jinping na mwenzake wa Marekani Joe BidenPicha: Kevin Lamarque/REUTERS

Kiongozi wa Wengi katika Baraza la Seneti Chuck Schumer akiongoza ujumbe wa watu sita, ndiye afisa wa ngazi ya juu wa Marekani kwenda China hivi karibuni, huku Washington ikijaribu kupunguza mvutano kati yake na Beijing.

Xi  alimwambia Schumer kwamba namna China na Marekanizinavyoshirikiana katika kukabiliana na ulimwengu wa mabadiliko na misukosuko ndivyo wataamua mustakabali na hatima ya wanadamu.

Soma pia:Marekani yaonya kuhusu kampeni ya upotoshaji wa China

Alisema alishawahi kusema mbele ya marais kadhaa kwamba kuna sababu 1,000 za kuboresha uhusiano kati ya China na Marekani. 

"Hakuna sababu hata moja ya kuuharibu uhusiano huu." Aliongeza kwamba uhusiano wa China na Marekani ni "muhimu kwa dunia" ya sasa.

Kwa upande wake kiongozi wa wengi kwenye seneti ya Marekani Chuck Schumer amesema Marekani na China kwa pamoja zitaujenga mustakabal wa dunia.

Schumer amesema nchi hizo zinapaswa kuundeleza uhusiano wao kwa njia ya busara.

Marekani na China lazima wamelize tofauti zao

Hapo awali mwanadiplomasia mkuu wa China Wang Yi alisema anatumai Washington na Beijing zinaweza kudhibiti tofauti zao "kwa busara zaidi".

Waziri wa Mambo ya Nje Wang aliuambia ujumbe wa seneti kwamba anatumai ziara yao ingesaidia pande hizo mbili "kudhibiti tofauti zilizopo kwa busara zaidi, kusaidia uhusiano kati ya nchi hizo mbili kurudi kwenye mkondo wa maendeleo chanya".

China | Der chinesische Präsident Xi Jinping trifft sich mit einer US-Kongressdelegation
Rais Xi Jinping akimlaki kiongozi wa wengi kwenye seneti ya Marekani Chuck SchumerPicha: Andy Wong/AP/picture alliance

Wang pia alisema anatumai "wangeielewa China kwa usahihi zaidi" baada ya safari hiyo, ambayo alisema inakuja wakati ulimwengu uko katika "kipindi cha mabadiliko".

"Changamoto hizi zote mbalimbali zinahitaji kushughulikiwa na jumuiya ya kimataifa, na China na Marekani zinapaswa kutekeleza wajibu wao,"  Wang alisema.

Mbali na kuushukuru ujumbe wa China Schumer Pia alisisitiza  masuala ya haki za binadamu na kukiri kusikitishwa na msimamo wa China juu ya mogogoro wa mashariki ya kati.

Soma pia:Biden: Kuna uwezekano wa kukutana na Rais wa China mwezi ujao

Beijing ilitoa wito siku ya Jumapili kwa pande zote kuonyesha "utulivu" na "kusitisha mapigano mara moja", bila kulaani hadharani shambulio la Wapalestina ambalo limesababisha mamia ya watu nchini Israel kuuawa.

"Ninaiomba China kusimama na watu wa Israel na kulaani mashambulizi haya mabaya," Schumer alimwambia Wang.

Schumer ndiye afisa wa ngazi ya juu zaidi wa Marekani kuzuru China huku Washington ikijaribu kupunguza mvutano na Beijing, ambao umepamba moto katika miaka ya hivi karibuni kuhusu kila kitu kuanzia biashara hadi haki za binadamu.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken, Waziri wa Fedha Janet Yellen na wa Biashara Gina Raimondo, pamoja na mjumbe wa hali ya hewa John Kerry, wote walifanya ziara nchini China mwaka huu.

Rais Joe Biden mnamo Ijumaa alisema kuwa anaweza kukutana na Xi huko San Francisco mnamo Novemba, lakini akaongeza kuwa hakuna chochote kilichopangwa.

China yachukua udhibiti wa ubalozi mdogo wa Marekani