1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Yaliyoandikwa na wahariri wa Ujerumani

Oummilkheir30 Novemba 2006

Mkutano wa NATO na kesi ya Mannesmann ndizo mada kuu magazetini hii leo

https://p.dw.com/p/CHUJ

Tuanze lakini na juhudi za NATO nchini Afghanistan.Gazeti la FRANKFURTER ALLGEMEINE linaadika:

„Jumuia ya kujihami ya magharibi NATO na mataifa yanayowajibika nchini Afghanistan wangepaswa kuutumia msimu wa baridi nchini humo ili kubuni mkakati wa kisiasa utakaofungamanisha shughuli za ujenzi mpya na harakati za kijeshi za kuimarisha usalama nchini humo.Ukishindikana au kama mkakati huo hautatekelzwa kikamilifu,basi hapatapita muda mrefu,watu wataanza upya kulaumiana.Serikali kuu ya Ujerumani imefanikiwa kuutetea msimamo wake:Angalao kwa sasa shughuli za vikosi vya jeshi la Ujerumani-Bundeswehr nchini Afghanistan,hazitabadilika.Misaada,ikihitajika itatolewa-kama hali namna ilivyo hivi sasa.Kilichosalia ni kusubiri na kuona kama hayo yatakidhi jukumu kubwa la Ujerumani.“

Gazeti la TAGESZEITUNG la mjini BERLIN-TAZ linasifu msimamo shupavu wa serikali kuu.Gazeti linaandika:

„Kansela hajaregeza kamba licha ya shinikizo la washirika watatu wa jumuia ya kujihami ya magharibi:Marekani,Canada na Uengereza:Vikosi vya jeshi la Ujerumani havitapelekwa kusini mwa Afghanistan.Kwa kila hali huo ni uamuzi wa maana.Wanajeshi wa Ujerumani wangehamishwa toka maeneo ya kaskazini basi hali hiyo ingehatarisha usalama na kukorofisha pia shughuli za kulijenga upya eneo hilo.Na zaidi ya hayo, hata wanajeshi wote 2700 wa Bundeswehr wakipelekwa,haimaanishi kama ndio watashawishi mustakbal wa mapambano dhidi ya wataliban.“

Hoja sawa na hizo zimetolewa pia na mhariri wa OSTTHÜRINGER ZEITUNG la mjini Gera anaeandika:

„Serikali kuu ya Ujerumani inastahiki kuvuliwa kofia kwa ukakamavu wake.Kwani nani asiyejua kwamba jumuia ya kujihami ya magharibi inadhibhitiwa na Marekani na wamerekani ndio wa mwanzo kupaza sauti kutaka wanajeshi waapelekwe kusini mwa Afghanistan.Rais George W. Bush,aliyepata pigo kubwa nyumbani kufuatia uchaguzi uliopita wa nusu njia,ameondoka mikono mitupu mjini Riga.Mkutano wa kilele wa Riga haukufanikiwa kubadilisha mengi katika juhudi za kugawana majukumu-kati ya vikosi katika nyanja za mapigano na vile vya kuijenga upya Afghanistan.Kwa hivyo ishara ya mshikamano iliyotokana na mkutano wa kilele wa Riga,mtu anaweza kusema ni dhaifu kupita kiasi.“

SÜDWEST PRESSE la mjini ULM linauangalia kwa ajicho la wasi wasi msimamo wa kansela Angela Merkel.Gazeti linaandika:

„Kilichosalia ni kutaraji tuu kwamba Angela Merkel ataendelea na msimamo huo huo hata kama shinikizo kutoka serikali ya Marekani litazidi kua kubwa.Mjini Riga,amesalimika kwa hoja za „dharura“,ingawa nchi nyengine zimeonyesha ukarimu mkubwa mbele ya Marekani.Lakini pindi NATO ikiendelea kukumbwa na shida nchini Afghanistan na kujitokeza hali sawa na ile ya Vietnam-hapo jumuia hiyo ya kujihami ya magharibi itabanwa kweli kweli.Hapatapita muda mrefu,pengine mkutano wa msimu wa kiangazi utakapoitishwa,suala hilo hilo litarejeshwa tena katika meza ya mazungumzo.Hapo tena tutajionea wenyewe kama kauli iliyotolewa na kansela Merkel mjini Riga bado ni thabiti.“

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani wamemulika pia kisa cha kusitishwa na korti ya Düseldorf, kesi mpya dhidi ya kampuni la MANNESMANN kwa kupokea bahshishi ya mamilioni ya yuro mkurugenzi mkuu wa benki mashuhuri ya Ujerumani Deutsche Bank Josef Ackermann na washtakiwa wenzake watano.

Kwa jumla wahariri wana mashaka kwasababu ya kusitishwa kesi hiyo bila ya kutolewa hukumu yoyote.Wanahisi Josef Ackermann kapitia mlango wa nyuma kutoka mahakamani.