1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ACCRA : Viongozi wa Afrika wajadili shirikisho

1 Julai 2007
https://p.dw.com/p/CBmn

Viongozi wa Umoja wa Afrika leo wameanza mkutano wa viongozi wa siku tatu kujadili mipango ya kuunda shirikisho la umoja huo ambalo litasaidia bara hilo maskini kabisa duniani kuwa na usemi zaidi katika jukwaa la kimataifa.

Akifunguwa mkutano huo Rais wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika Alpha Oumar Konare amesema azimio jipya la Umoja wa Mataifa linahitajika kuhakikisha kwamba Sudan inakubali uwekaji wa kikosi mchanganyiko cha Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa kilichokuwa kinasubiriwa kwa muda mrefu huko Dafur.

Huu ni mkutano wa tisa tokea kuazishwa kwa Umoja wa Afrika kuchukuwa nafasi ya Umoja wa Nchi Huru za Afrika OAU miaka mitano iliopita.

Wakati mikutano ya viongozi iliopita ilikuwa ikidhibitiwa na mizozo ya ndani ya nchi barani humo mkutano huu takriban moja kwa moja utajifunga katika kujadili kuanzishwa kwa kile kilichopachikwa jina kuwa ni Umoja wa Mataifa ya Afrika.

Miongoni mwa wanaoshiriki mkutano huo ni kiongozi wa Libya Muammar Gadafi ambaye anaonekana kuwa mpiga debe mkuu wa mradi huo ambaye angelipenda kuona matokeo yake kwenye sera ya pamoja ya mambo ya nje na ulinzi.