1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Baraza la Usalama latoa tamko dhidi ya Israel.

Halima Nyanza1 Juni 2010

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa leo limetoa wito wa kufanyika kwa uchunguzi usio na upendeleo juu ya Israel kushambulia meli iliyokuwa imepakiza misaada ya kibinadamu iliyokuwa ikielekea Gaza.

https://p.dw.com/p/NeVY
Waandamanaji sehemu mbalimbali duniani wamekjitokeza kupinga kitendo cha Israel kushambulia meli iliyopakiza wanaharakati na misaada kuelekea Gaza.Picha: AP
Tamko hilo la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ambalo limetolewa mwisho mwa kikao cha dharura, kilichofanyika kwa zaidi ya saa 12, limelaani kitendo hicho ambacho kimesababisha vifo vya watu 10 na wengine kadhaa kujeruhiwa. Taarifa iliyotolewa imesema Baraza la Usalama  limeizingatia maelezo ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa juu ya kufanyika kwa uchunguzi wa haraka, usio na upendeleo wa uhakika na wenye uwazi unaokidhi viwango vya kimataifa. Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limetaka pia kuachiliwa haraka kwa meli na wanaharakati wanaoshikiliwa na Israel. Awali Radio ya Israel iliripoti kuwa  Israel inawashikilia wanaharakati wapatao 480  na kwamba imewafukuza wengine 48. Balozi wa Mexico Claude Heller ambaye ndiye  mwenyekiti wa muda wa baraza la usalama amesema taasisi hiyo muhimu ya kimataifa imesisitizia wasi wasi wake juu ya hali ya kibinadamu iliyoko Gaza. Aidha taarifa hiyo imesisitizia pia kwamba ufumbuzi wa mzozo wa mgogoro wa Israel na Palestina ni kuwepo kwa mataifa mawili na kuelezea wasiwasi wake kutokana na tukio hilo kutokea wakati mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja yanaendelea kati ya pande hizo. Kwa upande wake Msaidizi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Oscar Fernandez-Taranco amesema shambulio hilo la umwagaji damu lililofanywa na Israel  lingeweza kuzuiwa. Katika kikao hicho cha baraza la Usalama, mataifa  ya kiarabu ambayo yalikuwa yakiungwa mkono na wanachama wengine wa baraza hilo ikiwemo Uturuki, wameitaka pia Israel kuondoa vizuizi ilivyoweka dhidi ya Gaza, haraka kuiachia meli hiyo na wanaharakati wa haki za binadamu na kuweza kuwaruhusu kupeleka bidhaa zao hizo, ukanda wa Gaza. Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Uturuki Ahmet amekielezea kitendo hichio cha Israel kama ni janga baya kutokea katika historia ya ubinadamu, mpaka kati ya ugaidi na taifa haupo tena. Wakati serikali mbalimbali duniani zikiendelea kuilaumu Israel kwa hatua yake hiyo, Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa litakutana leo kuzungumzia pia suala hilo mjini Geneva, huku Jumuia ya Kujihami ya NATO na mabalozi kutoka nchi 27 za Umoja wa Ulaya wakipanga pia kukutana kuzungumzia suala hilo mjini Brussels.  Waandamanaji kadhaa tayari wamejitokeza katika miji mbalimbali duniani kupinga kitendo hicho cha Israel. Wakati huo huo Israel imeonya leo kwamba itazuia meli zote za misaada kufika katika Ukanda wa Gaza, wakati wanaharakati, wakiahidi kufanya jaribio jipya kuhakikisha kuwa wanafika eneo hilo. Mwandishi: Halima Nyanza(afp,dpa) Imepitiwa na :Hamidou Oummilkheir: