1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bondia Pacquiao akubali ndoto yake ya Olimpiki imekwisha

19 Februari 2024

Manny Pacquiao "amehuzunishwa na kukatishwa tamaa" katika ndoto yake ya ndondi ya Olimpiki baada ya nguli huyo kunyimwa nafasi ya kushiriki katika michezo ya Paris ya mwaka huu.

https://p.dw.com/p/4ca2n
Manny Pacquiao
Bondia Manny Pacquiao Picha: picture-alliance/dpa/M. Nelson

Kamati ya Olimpiki ya Ufilipino imetangaza kwamba, Kamati ya Olimpiki ya Kimataifa ilikataa ombi maalum la Pacquiao kushiriki katika kinyangayiro hicho kwa kutobadili sheria zake kuhusu ukomo wa umri.

Pacquiao, 45, ambaye alitundika glavu zake mnamo 2021 kabla ya kinyang'anyiro cha urais bila mafanikio, alisema anaheshimu uamuzi wa IOC, ambayo ina kikomo cha umri wa miaka 40 kwa mabondia wanaoshiriki Olimpiki.

Soma pia: Timu ya wanamichezo wakimbizi katika Olimpiki

"Ingawa nimehuzunishwa sana na nimekatishwa tamaa, ninaelewa na kukubali sheria za kikomo cha umri," ilisema taarifa kutoka kwa Pacquiao, ambaye alishinda mataji ya dunia nane katika uzani tofauti wakati wa taaluma yake iliyomeremeta  iliyochukua zaidi ya robo karne.

Pacquiao alimaliza kazi yake ya ndondi mnamo Septemba 2021 akiwa na umri wa miaka 42 baada ya kupigana mara 72, kushinda mataji 12 ya ulimwengu.

Ufilipino mwaka jana iliomba IOC nafasi "maalum" kwa Pacquiao, ambaye hajawahi kupigana ngumi katika Olimpiki.

Nafasi hiyo ambayo kwa kawaida hutunukiwa wanariadha kutoka nchi ndogo ambao wanatatizika kupata nafasi katika Olimpiki kupitia kufuzu kwa kawaida.

Rais wa Kamati ya Olimpiki ya Ufilipino Abraham Tolentino amedai kwamba uamuzi wa IOC utainyima nchi hiyo " jukwaa la uhakika au dhahabu ya kwanza kabisa" katika ndondi za Olimpiki.

Las Vegas WBO
Bondia Manny Pacquiao akizipiga na Timothy Bradley - Aprili 09, 2016. Manny Pacquiao (kushoto) wa Ufilipino akimtazama Timothy Bradley wa Marekani baada ya kumpiga Knock out katika raundi ya tisa wakati wa ubingwa wa Kimataifa wa WBO uzito wa WelterweightPicha: picture-alliance/dpa/M. Nelson

Pacquiao alisema ataendelea kuwaunga mkono na kuwashangilia wanariadha wa Ufilipino wanaoshiriki michuano ya Olimpiki.

Pia aliwakumbusha mashabiki wake kwamba licha ya kustaafu kwake, anakusudia "kuleta fahari na heshima kwa nchi yangu ndani ya ulingo wa ndondi katika siku za usoni".

Soma pia: Mwanandondi Manny Pacquiao astaafu na kugeukia siasa

Msaidizi wa Pacquiao amethibitisha kwa waandishi wa habari kwamba Pacquiao atapigana na bondia wa kickboxer wa Thai, Buakaw Banchamek katika mechi ya maonyesho ya Aprili 20 huko Bangkok.

Mechi dhidi ya Muay Thai Buakaw itapigwa chini ya sheria za ndondi za kimataifa, msaidizi huyo alisema.