1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chadema kuandaa rasimu ya tume huru ya uchaguzi

Hawa Bihoga15 Februari 2019

Chadema ambacho ni chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania kimesema kitaandaa rasimu ya muundo wa tume huru ya uchaguzi ili ijadiliwe kabla ya uchaguzi mkuuu 2020.

https://p.dw.com/p/3DTQf
Tansania Chadema-Parteivorsitzender Freeman Mbowe 
Picha: DW/E. Boniphace

Chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania Chadema kimesema kinatarajia kuandaa rasimu ya muundo wa tume huru ya uchaguzi, kisha itapeleka kuwa mjadala wa kitaifa kabla ya uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka 2020.

Katika mkutano na waandishi habari uliodumu takriban saa zima, kaimu mwenyekiti wa chama hicho Profesa Abdallah Safari amesema kuwa kuna haja ya kufanya marekebisho katika tume ya uchaguzi ikiwemo kubadili vifungu vya katiba vinavyohusiana na tume, sheria ya uchaguzi ya mwaka 2002 pamoja na kanuni za uchaguzi wa urais na ubunge ili kuwa na uchaguzi huru na haki.


Hili linasababisha chama hicho kufikia maamuzi ya kuandaa rasimu ya tume huru ya uchaguzi ambayo itaandaliwa na kufikishwa katika kamati kuu ya chama hicho ambayo baadaye itawekwa hadharani na kufanywa mjadala wa kitaifa.

Chama cha Chadema chataka sheria ya uchaguzi kufanyiwa mageuzi.
Chama cha Chadema chataka sheria ya uchaguzi kufanyiwa mageuzi.Picha: DW/S. Khamis

Ameongeza kuwa chama hicho kina azma ya kuhakikisha wanapatikana washindi wa kweli katika chaguzi zinazofuata kuanzia wa serikali za mitaa ambao unatarajiwa kufanyika hapo baadaye mwaka 2019 ili kuondokana na swala la kulinda kura baada ya kukamilika kwa zoezi la kupiga kura.


Kadhalika chama hicho kilitazama pia mwenendo wa democrasia hasa katika ufanywaji wa mikutano ya wazi ya kisiasa kimesema wanajiandaa kuanza rasmi mikutano ya wazi licha ya zuio kutoka serikalini huku ajenda kubwa katika mikutano yao zitakuwa ni uminywaji wa demokrasia, ukiukwaji wa haki za binadamu pamoja na kukifikisha chama kwa wananchi wa mijini na vijijini.

Wakati chadema ikijiandaa kunyanyuka upya na kuanza mikutano tayari chama cha mapinduzi mara kadhaa kimeshuhudiwa kufanya mikutano na wanachama wake na wafuasi.


Mwandishi: Hawa Bihoga DW Dar es salamu

Mhariri: Josephat Charo