1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Dunia inasubiri kwa hamu mkutano kati ya Trump na Kim

Sekione Kitojo
11 Juni 2018

Rais wa  Marekani  Donald Trump  amesema  leo(11.06.2018) kwamba  mkutano wake  wa  kihistoria  na  kiongozi  wa  Korea  kaskazini Kim Jong Un nchini  Singapore unaweza  kuleta  matokeo mazuri.

https://p.dw.com/p/2zIma
USA Nordkorea - Donald Trump und Kim Jong Un - TV
Picha: picture alliance/AP Photo/L. Jin-man

Wakati  huo  huo maafisa wa  nchi  zote wanatafuta  kupunguza  tofauti  zao  juu  ya  vipi kumaliza  mkwamo  wa  kinyuklia  katika  rasi  ya  korea.

OAS-Generalversammlung | US-Außenminister Mike Pompeo
Waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Mike PompeoPicha: Getty Images/C. Somodevilla

Lakini  waziri wa  mambo  ya  kigeni  wa  Marekani  Mike Pompeo imetoa  ishara  ya  tahadhari   kabla  ya  mkutano  huo  wa  kwanza kufanyika  kati  ya  viongozi  wa  Marekani  na  Korea  kaskazini kesho  Jumanne, akisema  kwamba  inapaswa  kusubiri  kuona iwapo  Kim ni  mkweli juu  ya  kuwapo  kwake  tayari  kusitisha shughuli  za  kinyuklia.

Mazungumzo  ya  dakika  za  mwisho  kati ya  pande  hizo  mbili yalifanyika  katika  taifa  hilo  kwa  lengo  la  kuweka misingi ya mkutano  baina  ya  Trump  na  Kim, mkutano  ambao  ulikuwa hakuna  aliyeweza  kuufikiria  miezi  michache  iliyopita wakati viongozi  hao  wawili  walipokuwa  wakitupiana   matusi  na  vitisho ambavyo  viliongeza  hofu  ya  vita.

Singapur Kin Jong Un, Vivian Balakrishnan
Kiongozi wa Korea kaskazini akisalimiana na waziri wa mambo ya kigeni wa Singapore, Dr. Vivian BalakrishnanPicha: picture-alliance/AP Photo/Terence Tan

Lakini  baada  ya  wimbi  la  mazungumzo  ya  kukaribiana kidiplomasia  na  kupunguza  hali  ya  wasi  wasi  katika  miezi  ya hivi  karibuni, viongozi  hao  wawili  hivi  sasa  wanaelekea  kufanya kitendo  cha  kihistoria  cha  kushikana  mikono  ambapo  maafisa wa  Marekani  wanatumai  hatimaye  kutasababisha  katika  kusitisha kabisa  mpango  wa   kinyuklia  wa  Korea  kaskazini  ambao unaitishia  Marekani.

Akitoa  hali  ya  mkutano  huo  kwa  waandishi  habari  katika mkesha  wa  mkutano  wenyewe, waziri  wa  mambo  ya  kigeni  wa Marekani Mike Pompeo  alisema  mkutano  huo  unaweza  kutoa fursa  ambazo  hazikutarajiwa  kubadilisha  hali  ya  uhusiano  kati ya  nchi  hizo  mbili  na  kuleta  amani  na  usitawi , kwa  Korea kaskazini.

Kuondoa silaha za kinyuklia katika rasi ya Korea

Hata  hivyo, hakuzungumzia  kwa  hamasa  kubwa  uwezekano  wa upatikanaji wa  mapatano  ya  haraka   na  kusema  mkutano  huo wa  kilele  unapaswa  kuweka  mwongozo kwa  ajili  ya  "kazi  ngumu inayofuata", akisisitiza  kwamba  Korea  kaskazini  inapaswa kuelekea  katika  kuondoa  kabisa  bila  kurudi  nyuma   silaha za  kinyuklia.

"Kutokana  na  makubaliano  hafifu ambayo Marekani ilifikia katika miaka  iliyopita, rais atahakikisha hakuna makubaliano yatakayofikiwa ambayo yatakosa  kuzungumzia kwa  kina, kitisho cha  Korea kaskazini. Lengo kuu la kuwa na mahusiano  ya kidiplomasia  na  Korea  kaskazini  halijabadilika.

Singapur: Donald Trump an der Paya Lebar Air Base
Rais Donald Trump akiwasili nchini SingaporePicha: picture-alliance/AP Photo/E. Vucci

Mpango kamili utakaoweza  kufanyiwa  uchunguzi wa  kina  wa  kuondoa  kabisa silaha za  kinyuklia katika  rasi ya  Korea ni  matokeo pekee ambayo Marekani itayakubali. Vikwazo  dhidi  ya  Korea  kaskazini vitaendelea  hadi  pale nchi  hiyo itakapokamilisha  kuondoa  kabisa mpango wake  wa  silaha za  kinyuklia. Iwapo diplomasia haitakwenda  katika  njia  sahihi  na  tunamatumaini kwamba itaendelea  vizuri,  hatua hizo zitaongezeka."

Korea  kaskazini  hata  hivyo  imeonesha  nia hafifu  ya  kuachana na  silaha  zake  za  kinyuklia ambazo  inaziona  kuwa  muhimu  kwa ajili  ya  uhai  wa  utawala  wa   ukoo  wa  Kim. Ikulu  ya  Marekani ya  White House  ilisema  baadaye  kuwa  majadiliano  na  Korea kaskazini  yamekwenda  kwa  kasi  sana  kuliko  ilivyotarajiwa  na Trump  ataondoka  Singapore usiku  wa  jumanne  mara  baada  ya mkutano  huo. Alipangiwa  hapo  mapema kuondoka  Jumatano.Naye Kim anatarajiwa  kuondoka kurudi Pyongyang  Jumanne  jioni.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / rtre

Mhariri: Mohammed Abdul Rahman