1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maduro awashutumu waangalizi wa uchaguzi kutoka Ulaya

Lilian Mtono
29 Novemba 2021

Rais wa Venezuela Nicolas Maduro ameushutumu ujumbe wa waangalizi wa uchaguzi kutoka Umoja wa Ulaya akisema kuwa walikuwa ni majasusi huku akiwatupia lawama kuwa wanaangazia namna ya kuuchafua uchaguzi wa mikoa.

https://p.dw.com/p/43c1n
Nach den Regionalwahlen in Venezuela
Picha: Javier Vegas/AP/picture alliance

Rais Nicolas Maduro ameushutumu ujumbe huo wa Umoja wa Ulaya akisema hawakwenda kufuatilia mambo yanavyokwenda na badala yake walikwenda kujaribu kuutia doa mchakato wa uchaguzi na hali ya maisha na kisiasa nchini Venezuela lakini hawakufanikiwa. Alisema hayo kwenye hotuba yake kupitia kituo cha televisheni cha taifa.

Walikuja kupeleleza mchakato wa Venezuela na kutafuta kipengele kimoja cha kukikuza, kukizidisha na kujaribu kuutia doa uchaguzi. Lakini Umoja wa Ulaya haukuweza kuitia doa Venezuela na mchakato wa uchaguzi umekuwa mzuri wa ushindi."

Maduro aliongeza kuwa Umoja wa Ulaya usingeweza kuuchafua mchakato wa uchaguzi, huku akikana madai kwamba uligubikwa na udanganyifu. 

Ujumbe huo wa Umoja wa Ulaya hautaka kujibu chochote walipotafutwa kuzungumzia matamshi hayo.

Uchaguzi wa mikoa nchini Venezuela umefanyika mwishoni mwa wiki iliyopita, na ujumbe huo wa Umoja wa Ulaya ulisema siku ya Jumanne kwamba ulifanyika katika mazingira mazuri zaidi ikilinganishwa na huko nyuma.

Venezuela Isabel Santos, Mitglied des Europäischen Parlaments und Chefbeobachterin der EU-Wahlbeobachtungsmission 2021
Mkuu wa ujumbe wa Umoja wa Ulaya uliofuatilia uchaguzi nchini Venezuela Isabel dos Santos ameeleza wasiwasi wake juu ya ukiukwaji kwenye uchaguzi huo.Picha: Ariana Cubillos/AP Photo/picture alliance

Lakini hata hivyo kiongozi wa ujumbe huo Isabel Santos alielezea wasiwasi kuhusiana na uvunjwaji wa sheria akitolea mfano hatua za kiholela za kuwazuia baadhi ya wagombea, kuchelewa kufunguliwa kwa vituo vya kupigia kura na kile walichokitaja kama matumizi ya kupindukia ya rasilimali za serikali katika kampeni.

Soma Zaidi: Mgogoro wa kiisiasa wazidi makali Venezuela

Upinzani washindwa vibaya.

Uchaguzi huo wa Venezuela ulikuwa ni wa kwanza katika kipindi cha miaka 15, kushuhudiwa na wajumbe kutoka Umoja wa Ulaya. Serikali ya Maduro, ambayo ilishinda kwenye uchaguzi wa mwaka 2018 kwa kiasi kikubwa haitambuliwi na jumuiya ya kimataifa. Ripoti kamili kuhusu uchaguzi huu inatarajiwa kutolewa katika kipindi cha miezi miwili ijayo.

Wanasiasa wa upinzani pia waliwania kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2017 na kuhitimisha kipindi cha kususia kushiriki uchaguzi. Hata hivyo walizidiwa nguvu na kufanikiwa kuchukua viti vitatu tu kati ya 23 vya ugavana na 17 vya Umeya, huku chama tawala kukushinda viti 210. Lakini baadhi ya maeneo bado hayajafanya uchaguzi wa umeya na jimbo la Barina nalo bado halijachagua gavana.

Awali ilielezwa kwamba rais Maduro angekutana na kuzungumza na magavana kutoka upande wa upinzani katika kipindi cha masaa kadhaa yajayo, ingawa hakukutolewa maelezo zaidi kuhusiana na mikutano hiyo.

Mashirika: RTRE/AFPE