1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mafahali wa Syria wakutana katika meza ya mazungumzo Geneva

Oumilkheir Hamidou
30 Oktoba 2019

Wawakilishi wa pande zinazopigana vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Syria wanaketi katika meza ya mazungumzo kwa mara ya kwanza baada ya kupita miaka minane na nusu ya umwagaji damu, mjini Geneva kutunga katiba mpya.

https://p.dw.com/p/3SBPD
Schweiz PK in Genf Mevlut Cavusoglu, Mohammad Javad Zarif und Sergei Lawrow
Picha: Reuters/D. Balibouse

Jumatano mchana wajumbe 150, 50 kutoka kila upande, serikali, upande wa upinzani na mashirika ya kiraia wataanza mazungumzo yatakayosimamiwa na Umoja wa Mataifa mjini Geneva.

Urusi na Iran, washirika wa serikali ya Bashar al Assad, na Uturuki inayowaunga mkono wapinzani wanaiangalia kamati ya kutunga katiba kama fursa iliyojitokeza ya kuleta hali ya kuaminiana na kufungua njia ya kuanzisha utaratibu wa kisiasa utakaomaliza mzozo wa Syria.

"Tunazihimiza pande zote zinazohusika zifikie makubaliano" amesema waziri wa mambo ya nchi za nje wa Urusi Sergei Lavrov katika mkutano na waandishi habari, katika wakala ya Umoja wa Mataifa mjini Geneva Uswisi, bada ya kukutana na mawaziri wenzake wa Uturuki na Iran pamoja pia na mjumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Syria Geir Pedersen.

Katika wakati ambapo waziri wa mambo ya nchi za nje wa Iran Mohammad Javad Zarif anashauri maadola hayo matatu makuu ya kikanda yasiingilie kati katika utaratibu wa kutunga katiba, waziri mwenzake wa Uturuki Mevlut Cavusglu anasema ingawa anajiwekea matumaini mema lakini anatambua pia kwamba mazungumzo yatakuwa magumu.

Kumbukumbu za miaka zaidi ya minane na nusu ya vita vya wenyewe kwa wenyewe
Kumbukumbu za miaka zaidi ya minane na nusu ya vita vya wenyewe kwa wenyewePicha: DW/K. Zurutuza

Mada tete inahusu kuachiliwa huru waungwa wa vita

Madola hayo matatu makuu ya kikanda hayatowakilishwa katika mazungumzo ya pande zinazohasimiana nchini Syria ambayo hayakuwekewa ratiba maalum mjini Geneva.

Duru kadhaa za mazungumzo yaliyosimamiwa na Umoja wa Mataifa kuhusu Syria zilishindwa hapo awali kuleta tija kwakua wawakilishi wa serikali na wale wa upande wa upinzani walishindwa kuwajibika ipasavyo mazungumzoni.

Mapema wiki hii mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa katika mzozo wa Syria, Geir Pedersen alisema kamati ya kutunga katiba pekee haitotosha kuupatia ufumbuzi mzozo wa Syria."Mbali na mazungumzo hayo, hali ya kuaminiana inahitajika na hasa katika juhudi za kusaka ufumbuzi kuhusu maelfu ya wafungwa wa vita na mateka wa vita" amesema mwanadiplomasia huyo wa Umoja wa mataifa.

Zaidi ya watu 370 000 wameuwawa tangu vita vya wenyewe kwa wenyewe viliporipuka mwaka 2011 nchini Syria.