1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MAGAZETI YA UJERUMANI JUU YA NJAA KATIKA AFRIKA MASHARIKI

19 Agosti 2011

Magazeti ya Ujerumani yaizingatia hali ya Afrika Mashariki.

https://p.dw.com/p/12JWC
Waziri Mkuu wa Kenya Raila Odinga akizungumza na Waziri Dirk Niebel wa Ujerumani.Picha: DW

Wiki hii vile vile magazeti ya Ujerumani yameandika juu ya janga la njaa kwenye eneo la Pembe ya Afrika.

Gazeti la Frankfurter Allgemeine limefanya mahojiano na mwenyekiti wa shirika la misaada ya chakula la Ujerumani bibi Bärbel Dieckmann aliepata fursa ya kuitembelea kambi ya Dadaab nchini Kenya.

Katika mahojiano hayo bibi Dieckmann amesema alisikitishwa sana na hali aliyoiona kwenye kambi hiyo.Ameeleza kuwa watu karibu 400,000 kwenye kambi hiyo hawana matumaini yoyote juu ya siku za usoni. Mwenyekiti huyo wa shirika la misaada ya chakula bibi Dieckmann ametamka kuwa njia pekee ya kuwapa watu wa Somalia matumaini ni kufikiwa suluhisho la kisiasa nchini humo.

Gazeti la die tageszeitung pia liemandika juu ya hali ya eneo la Pembe ya Afrika. Gazeti hilo limearifu kuwa waziri wa ushirikiano wa maendeleo wa Ujerumani Dirk Niebel ameyashangaza mashirika ya misaada. Waziri huyo alitangaza nyongeza ya Euro milioni 118 kwa ajili ya watu wa eneo la Pembe ya Afrika wanaokabiliwa na janga la njaa. Waziri Niebel aliitangaza nyongeza hiyo jumatatu iliyopta mjini Nairobi baada ya kufanya ziara kwenye kambi ya Dadaab. Hadi wakati huo Ujerumani ilikuwa imeshatoa kiasi cha Euro milioni 35 kwa ajili ya watu wa eneo la Pembe ya Afrika.

Lakini nyongeza hiyo imeyakuta mashirika ya misaada bado hayajajitayarisha. Gazeti la die tageszeitung limemnukulu msemaji wa Shirika la Chakula la Umoja wa Mataifa,WFP bibi Katharina Weltecke akisema kuwa shirika lake halijui ni kiasi gani cha fedha hizo kitakabidhiwa kwa shirika lake na ni kiasi gani kitatumika kwa ajili ya miradi ya muda mrefu.

Gazeti la der Stern pia limechapisha makala juu ya njaa katika Afrika Mashariki. Gazeti hilo linasema katika makala yake watu katika sehemu hiyo wanakabiliwa na maafa ya njaa , siyo tu kwa sababu ya ukame. Sera za nchi za mgharibi pia zimechangia. Gazeti la der Stern linasema kile kinachoitwa misaada ya maendeleo kinachangia katika kusasabisha maafa ya njaa katika eneo la pembe ya Afrika. Gazeti hilo linasema misaada hiyo ya maendeleo inaingia katika mikono ya madikteta na vile vile inawafanya watu wajenge ulemavu wa kutegemea misaada.

Aliekuwa Rais wa Misri Hosni Mubarak wiki alifikishwa tena mahakamani mjini Cairo kujibu tuhuma za mauaji.

Hizo ni habari zilizoandikwa wiki hii na gazeti la Berliner Zeitung. Lakini gazeti hilo linauliza maswali kadhaa juu ya kesi ya Mubarak.Gazeti la Berliner Zeitung linatilia maanani kwamba haijawahi kutokea katika historia ya hivi karibuni nchini Misri kwamba mtawala anafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazomkabili. Gazeti hilo linasema watu wengi wa Msiri wanakubalina kwamba Mubarak anayo maswali ya kuyajibu juu ya utawala wake wa miaka karibu 30 . Lakini gazeti hilo linauliza iwapo ni sawa kumfikisha mzee huyo mgongwa mbele ya mahakama?

Gazeti la Süddeutsche Zeitung pia limechapisha makala juu ya kesi ya Mubarak. Gazeti hilo limeweza kubaini kwamba, watetezi wa wahanga wa uhalifu wa Mubarak wanajitokeza kwenye kesi hiyo kama watu wasiokuwa na nidhamu, wakati mawakili wa Mubarak wanaonyesha kuwa wanao mkakati wa hekima.Gazeti la Süddetsche linasema watetezi wa wahanga wa uhalifu wa Mubarak hawaheshimu mahakama. Wanapiga kelele na kusukumana mbele ya hakimu. Gazeti hilo limearifu kwamba jumanne iliyopita watetezi hao zaidi ya mia moja walikwenda kuhudhuria siku ya pili ya kesi ya Mubarak. Lakini watetezi hao hawakonyesha iwapo walikuwa na mkakati wowote.

Gazeti la die tageszeitung wiki hii pia limeripoti juu ya kutekwa nyara mfanyakazi wa shirika la misaada kutoka Italia. Mfanyakazi huyo alitekwa nyara katika jimbo la Darfur,magharibi mwa Sudan.

Maalfu ya watu walifanya maandamano ya kupinga kukiukwa haki za binadamu, rushwa na umasikini nchini Malawi. Hizo ni habari zilizochapishwa na gazeti la Neues Deutschland. Watu 17 waliuawa, 58 walijeruhiwa na wengine 275 walitiwa ndani na polisi wa Rais Bingu wa Mutharika.

Mwandishi/Mtullya abdu/Deutsche Zeitungen.

Mhariri: Miraji Othman