1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mahakama ya Katiba Kongo yaidhinisha ushindi wa Tshisekedi

Saleh Mwanamilongo
9 Januari 2024

Felix Tshisekedi atarajiwa kuanza muhula wa pili baada ya Mahakama ya Katiba nchini Kongo kuidhinisha matokeo ya uchaguzi yaliompa ushindi kwa asilimia sabini na tatu.

https://p.dw.com/p/4b2bh
Demokratische Republik Kongo | Wahlkampf Präsident Felix Tshisekedi
Picha: REUTERS

''Bwana Tshisekedi Tshilombo Felix Antoine amechaguliwa kuwa rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kwa wingi wa kura zilizopigwa,'' alisema Kamuleta Badibanga Dieudonne, Jaji Mkuu wa Mahakama ya Katiba nchini Kongo.

Awali, Mahakama ilitupilia mbali hoja ya mgombea wa upinzani Theodore Ngoy yakutaka uchaguzi urudiwe, mahakama ilisema hoja hiyo haina msingi. Ngoy ambaye alipata chini ya asilimia moja ya kura, ndiye mgombea pekee aliyekata rufaa.

Upinzani kuendelea kupinga matokeo ya uchaguzi

Baadhi ya wagombea wengine wa urais  wakiwemo Moïse Katumbi, Martin Fayulu na Denis Mukwege wao wametaka matokeo ya uchaguzi yabatilishwe lakini walikataa kufungua shauri mahakamani wakadai chombo hicho kinaendesha kazi zake kwa misingi ya upendeleo. Wanalalamika kuwa uchaguzi huo mkuu uligubikwa na hitilafu nyingi na matokeo yake yalikuwa ya udanganyifu.

Tshisekedi, mwenye umri wa miaka 60, ataapishwa mwishoni mwa mwezi huu wa Januari kwa muhula wa pili wa miaka mitano.