1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marais wa nchi za maziwa makuu wakutana kuhusu usalama

Saleh Mwanamilongo
7 Oktoba 2020

Marais wa nchi nne za kanda ya maziwa makuu wanashiriki mkutano wa kilele ambao uliitishwa na rais Felix Tshisekedi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

https://p.dw.com/p/3jYLA
Ruanda Uganda Konflikt Treffen Grenzstreitigkeiten in Katuna
Picha: Presidential Press Unit of Uganda

Marais wa nchi nne za kanda ya maziwa makuu wametarajiwa kushiriki leo kwenye mkutano wa kilele wa siku moja ambao uliitishwa na rais Felix Tshisekedi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Mkutano huo unalenga kujadili maswala ya kiusalama nchini Congo na katika nchi jirani. hata hivyo rais wa Burundi Evariste Ndayishimiye hatohudhuria mkutano huo. 

Mkutano huo ambao uliakhirishwa mara kadhaa, hatiamae utafanyika kwa njia ya video. Mwenyeji wa mkutano huo, rais Felix Tshisekedi ametarajiwa kuwashawishi marais wenzake Paul Kagame wa Rwanda, Yoweri Museveni wa Uganda na Joao Lourenco wa Angola kuhusu jitihada za pamoja kwa ajili ya usalama hasa katika  majimbo ya Kivu ya kaskazini, Kivu ya kusini na Ituri.

Wataalamu na mawaziri wa mambo ya nje walijadili ajenda ya mkutano huo kabla ya kiako cha ma rais cha hivi leo. Marie Ntumba Nzeza waziri wa mambo ya nje wa Congo amesema kwamba marais hao watajadili pia kuhusu janga la virusi vya Corona, maswala ya kibiashara  na uhusiano bora.

'' Sababu na lengo la mkutano huo wa kilele uliotishwa na rais Felix Tshisekedi,ni kuweko na tathmini ya kina ya viongozi wa Rwanda,Uganda,Angola,Kongo na Burundi, kuhusu hali jumla kwenye kanda hii na hasa ustawi wake.''

Burundi yataka kuwepo na vikao vya nchi mbili

  Duru kwenye wizara ya mambo ya nje ya Kongo zinaelezea kwamba rais wa Burundi ,Evariste Ndayishimiye hato shiriki kwenye mkutano huo licha ya kualikwa. Siku mbili zilizopita waziri wa mambo ya nje wa Congo, alifanya ziara mjini Bujumbura katika juhudi za kutaka kushiriki kwa rais Ndayishimiye.

Raïs wa Burundi, Evariste Ndayishimiye
Raïs wa Burundi, Evariste NdayishimiyePicha: Getty Images/AFP/T. Nitanga

Wizara ya mambo ya nje ya Burundi ilielezea umuhimu wa kuweko kwanza na vikao baina ya Kongo na Burundi kuhusu maswala ya pamoja ,kabla ya mkutano huo wa kilele.

Mashambuzi yaendelea Kivu na Ituri

Rais Tshisekedi yuko ziarani mjini Goma,jimboni Kivu ya Kaskazini, toka Jumatatu. Ziara hiyo imekuja baada ya mfululizo wa mashambulizi ya wapiganaji wa ADF katika maeneo ya mji  wa Beni ambako makumi ya raia waliuliwa siku za hivi karibuni.

Serikali iliendesha mazungumzo na baadhi ya makundi ya wapiganaji huko Kivu ya kaskazini ,Kivu ya kusini na Ituri,ilikuyashawishi kuweka chini silaha. Shirika la watoto la umoja wa mataifa,UNICEF,limesema hapo jana kwamba watoto 91 waliuliwa mnamo kipindi cha miezi sita iliopita kufuatia machafuko kwenye jimbo la Ituri.