1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSomalia

Mikoa ya Somalia yapuuza amri ya kufunga balozi za Ethiopia

6 Aprili 2024

Majimbo mawili ya Somalia ya Somaliland na Puntland yamekataa maelekezo ya serikali kuu ya kuzifunga balozi ndogo za Ethiopia kwenye maeneo yao katikati mwa mzozo unaopamba moto kwenye eneo la Pembe ya Afrika.

https://p.dw.com/p/4eURh
Rais Hassan Sheikh Mohamud wa Somalia
Rais Hassan Sheikh Mohamud wa SomaliaPicha: REUTERS

Mnamo siku ya Alhamisi, Somalia ilimpatia Balozi wa Ethiopia saa 72 kuondoka nchini humo na kumrejesha nyumbani balozi wake wa mjini Addis Ababa, baada ya kuituhumu Ethiopia kuingilia masuala yake ya ndani.

Hapo jana serikali mjini Mogadishu pia iliamuru ofisi  ndogo za ubalozi wa Ethiopia kwenye jimbo lililojitenga la Somaliland na lile lenye utawala wake wa ndani la Puntland zifungwe ndani ya siku saba.

Hata hivyo wizara ya habari ya Somaliland imepuuza amri hiyo ikisema ubalozi huo wa Ethiopia ndani ya jimbo hilo haukufunguliwa kwa ruhusa ya Somalia na kwa msingi huo hautafungwa. Msimamo sawa na huo umetolewa pia na jimbo la Puntland.

Somalia imetumbukia kwenye mzozo na Ethiopia kutokana na mkataba uliotiwa saini kati ya serikali ya Addis na jimbo la Somaliland wa kuiruhusu Ethiopia kutumia sehemu yake ya bahari.

Somalia inasema mkataba huo ni batili na ni ukiukaji wa uhuru wake.