1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ripoti ya utafutaji mafuta Zanzibar kutolewa mwaka huu

Salma Said30 Septemba 2019

Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohammed Shein amesema matokeo ya utafutaji wa mafuta na gesi asilia visiwani Zanzibar yatatolewa mwaka huu.

https://p.dw.com/p/3QTbb
Tansania | Politiker besuchen die erste Tourismusausstellung in Sansibar
Picha: DW/S. Said

Kazi ya utafutaji wa nishati ya mafuta na gesi asilia Zanzibar imeingia katika hatua nyengine baada ya Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohammed Shein kusema kwamba matokeo ya uchambuaji wa taarifa zilizopatikana kutokana na utafutaji huo utatolewa mwaka huu. 

Kauli hiyo ameitoa jana wakati aliporudi safari yake ya wiki moja katika nchi za Falme za kiarabu ambapo pamoja na kazi nyengine alizungumzia suala la utafutaji wa mafuta na gesi asilia, huku akisisitiza kuwa yeye hajavunja katiba katika uamuzi wake wa utafutaji na hatimae uchimbaji wa nishati hiyo.

Tangu Zanzibar kutiliana saini mkataba na kampuni ya RAKGAS kwa ajili ya utafutaji na uchimbaji wa mafuta mwaka jana kumekuwepo na kauli mbali mbali miongoni mwa baadhi ya viongozi, wanasheria na mitandao ya kijamii kwamba utafutaji huo unakwenda kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutokana na suala hilo la mafuta na gesi asilia linabaki kuwa ni mali ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania kwa mujibu wa katiba.

Mwana jana, Zanzibar ilitiliana saini mkataba na kampuni ya RAKGAS kwa ajili ya utafutaji na uchimbaji wa mafuta.
Mwana jana, Zanzibar ilitiliana saini mkataba na kampuni ya RAKGAS kwa ajili ya utafutaji na uchimbaji wa mafuta.Picha: picture-alliance/AP Photo/T. Camus

Dk. Shein alisema tangu Zanzibar kuamua kutafuta rasilimali ya mafuta, kampuni ya RAKGAS tayari imeshafanya kazi nzuri na kwamba kuna muelekeo mzuri lakini akataka wananchi wawe na subira kwa sababu utafutaji wa mafuta huchukua muda mrefu.

Katika mazungumzo yake na viongozi wa nchi hizo Dk Shein aligusia katika masuala ya kujenga uchumi imara wa Zanzibar ambapo amesema serikali ya Zanzibar itaimarisha uwanja wake wa ndege pamoja na kujenga bandari mpya kwa kutumia fedha zake wenyewe baada ya juhudi za kupata mkopo kutoka nje kugonga mwamba kutokana na Serikali ya Muungano kukataa kudhamini mkono huo.

Kukosekana kwa mkopo huo umechelewesha miradi mikubwa mitatu ikiwemo ujenzi wa bandari mpya ya mpiga duri, uwanja wa ndege wa kimataifa na baadhi ya barabara za Pemba, ambapo Mara kwa mara wajumbe wa baraza la wawakilishi wamekuwa wakihoji sababu za Serikali ya Tanzania kusita kudhamini mikopo hiyo ambayo huchelewesha maendeleo na ustawi wa Zanzibar jambo ambalo wachambuzi husema Zanzibar kutokuwa na Mamlaka yake ya kujiamulia ni miongoni mwa kero kubwa za Muungano.