1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

SADC yahimiza kura zihesabiwe upya Congo Kinshasa

Oumilkheir Hamidou
14 Januari 2019

Jumuia ya Maendeleo ya Mataifa ya Kusini mwa Afrika-SADC inaitia kishindo korti ya katiba kwa kutoa wito wa kuundwa serikali ya umoja wa kitaifa na kura kuhesabiwa tena katika jamhuri ya kidemokrasi ya Congo

https://p.dw.com/p/3BVIQ
Edgar Lungu Zambia Präsident
Picha: picture-alliance/P.Wojazer

Mwenyekiti wa jumuia ya Maendeleo kusini mwa Africa SADC, rais Edgar Lungu wa Zambia amesema jumuia hiyo inazingatia kwa makini shaka shaka zilizotolewa kuhusiana na matokeo ya awali yaliyotangazwa na kutilia mkazo kura zihesabiwe upya akisema hiyo ndio njia pekee ya kutuliza wasi wasi wa aliyeshinda na pia wa walioshindwa.

Kwa kutoa wito wa kuhesabiwa upya kura za uchaguzi wa rais, na kuwataka viongozi wa jamhuri ya kidemokrasi ya Congo wazingatie uwezekano wa kufikia makubaliano ya kisiasa kwa njia ya maridhiano, jumuia ya SADC inakwenda mbali zaidi kupita jumuia ya kimataifa..Jumuia ya Maendeleo kusini mwa Afrika SADC inayozijumuisha pia Afrika Kusini na Angola miongoni mwa wanachama wake ina masilahi makubwa ya kiuchumi katika jamhuri ya kidemokrasi ya Congo ambayo pia ni mwanachama..Jumuia ya SADC ilituma wasimamizi katika uchaguzi mkuu decemba 30 iliyopita na kuashiria baadae" uchaguzi huo umepita vizuri."

Tume ya uchaguzi CENI ikizungumza na waandishi habari
Tume ya uchaguzi CENI ikizungumza na waandishi habariPicha: DW/Wendy Bashi

Kura zihesabiwe upya

Umoja wa Ulaya umetoa wito wa kuchapishwa ripoti ya kutoka vituo vyote ambako kura zilihesabiwa nayo Marekani ikataka ufafanuzi na kuzisihi pande zote zinazohusika ziendeleze hali ya utulivu. Wito kama huo umetolewa pia na Umoja wa Afrika.

Shaka shaka za jumuia ya kimataifa zinatokana na msimamo wa kanisa katoliki-taasisi yenye ushawishi mkubwa kabisa nchini humo, ililoutaka Umoja wa Mataifa uchapishe ripoti zote za uchaguzi ili kuondowa shaka shaka.

Kwa mujibu wa mkutano wa baraza la taifa la maaskofu wa jamhuri ya kidemokrasi ya Congo-CENCO, matokeo yaliyotangazwa na tume huru ya uchaguzi CENI hayalingani na matokeo yaliyokusanywa na wasimamizi 40.000 wa taasisi hiyo.

 

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AFP

Mhariri:Iddi Ssessanga