1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MichezoIvory Coast

Taifa Stars yatupwa nje ya michuano ya AFCON

Tatu Karema
25 Januari 2024

Timu ya taifa ya Tanzania taifa stars imetupwa nje ya michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika AFCON baada ya kutoka sare tasa na Jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo

https://p.dw.com/p/4be4o
Wachezaji wa timu ya taifa ya Tanzania, taifa stars wakifanya mazoezi mnamo Novemba 11, 2021
Timu ya taifa ya Tanzania, taifa starsPicha: Ericky Boniphase

Jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo ambayo imejikatia tiketi ya hatua ya mtoano ikiwa na alama 3 sasa itakuwa na kibarua dhidi ya Misri mnamo Januari 28 . 

Ivory Coast yapata mwanya wa kusonga mbele

Katika kundi hilo F, Morocco imeifunga Zambia bao moja kwa nunge. Ushindi huo umeipatia nafasi Ivory Coast mwenyeji wa michuano hiyo kufuzu kama moja ya timu nne bora zilizomaliza katika nafasi ya tatu.

Soma pia:Ivory Coast ukingoni mwa kutolewa nje ya michuano ya AFCON

Ivory Coast watavaana na Simba wa Teranga Senegal Jumatatu ijayo, huku Morocco wakiwa na miadi na Afrika Kusini siku ya Jumanne.

Tunisia yatupwa nje ya michuano ya AFCON

Tunisia nayo imepigwa kumbo na kutolewa nje ya michuano hiyo baada ya kutoka sare ya 0-0 na Afrika Kusini inayojulikana kwa jina la utani kama bafana bafana katika mechi ya mwisho ya Kundi E mjini Korhogo.

Soma pia:Bao la dakika za mwisho la Zambia lainyima Tanzania ushindi wake wa kwanza AFCON

Tunisia, ambayo imeorodheshwa ya tatu katika orodha ya ubora wa soka barani Afrika, imekuwa timu ya pili miongoni mwa mataifa kumi bora baada ya Algeria kutolewa nje baada ya mechi za makundi.

Afrika Kusini kukutana na Moroko

Kufuatia matokeo hayo, Afrika Kusini imetinga hatua ya mtoano ya timu 16 bora ya michuano hiyo ya AFCON. Afrika Kusini ilikuwa inahitaji alama moja tu ili kufuzu.

Mashabiki wa timu ya taifa ya Afrika Kusini almaarufu bafana bafana wakishangilia wakati wa mechi kati ya timu hiyo na Mexico katika uwanja wa michezo mjini Johannesburg mnamo Juni 11, 2010
Mashabiki wa timu ya taifa ya Afrika Kusini almaarufu bafana bafanaPicha: AP

Bafana Bafana itakutana na washindi wa kundi F Moroko mjini San Pedro nchini Ivory Coast siku ya Jumanne.

Namibia yafuzu kusonga mbele

Wakati huo huo, timu ya taifa ya Namibia imefuzu kwa mara yake ya kwanza katika hatua ya mtoano kwa kutoka sare tasa na Mali iliyomaliza ya kwanza katika kundi E ikiwa na alama 5 muhimu.

Soma pia:Moroko yaichabanga Tanzania 3-0 AFCON

Namibia inayofahamika kama the brave warriors itachuana na washindi wa kundi D Angola wakati Mali ikipambana na Burkina Faso.

Mechi ya Brave warriors dhidi yaAngola , itachezwa siku ya Jumamosi mjini Bouake wakati mechi kati ya Mali na Burkina Faso ikitifua vumbi mjini Korhogo siku ya Jumanne.

Algeria yamtimua kocha wake Djamel Belmadi

Algeria imemtimua kocha wao Djamel Belmadi jana baada ya washindi hao mara mbili wa kombe la mataifa ya Afrika kutolewa nje ya michuano ya AFCON baada ya mechi za makundi.

Soma pia:Algeria yabanwa na Angola katika mechi ya ufunguzi AFCON

Muhula wa Belmadi ulifika mwisho kabla muda wake kufuatia matokeo ya kushtusha ya kufungwa na Mauritania mechi yao ya mwisho.

 Hakim Ziyech afunga bao la kwanza la Moroko wakati wa mechi yake na Zambia nchini Ivory Coast Januari 24, 2024
Mechi kati ya Morocco na Zambia nchini Ivory CoastPicha: Sunday Alamba/AP Photo/picture alliance

Rais wa shirikisho la soka la Algeria Walid Sadi ameandika kwenye ukursa wake wa X kwamba alikutana na kocha Djamel Belmadi kujadili athari za kutolewa nje ya mashindano ya AFCON, na wakafikia makubaliano ya kufikisha mwisho mahusiano yao na kufuta mkataba wake.

Makocha wengine waliotimuliwa na timu zao

Kutimuliwa kwa Belmadi kunafuatia hatua ya Ivory Coast kumfuta kazi kocha wao, Jean-Louis Gasset na Ghana nao kumtimua kocha wao Chris Hughton.

Soma pia:AFCON: Ivory Coast yafungua dimba kwa ushindi wa mabao mawili

Michuano hiyo ya AFCON itachukuwa mapumziko ya siku mbili leo na kesho na kuendelea tena siku ya Jumamosi Januari 27 kati ya Super eagles ya Nigeria na Cameroon.