1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania: Ukeketaji sasa unafanywa kwa vichanga

Admin.WagnerD6 Februari 2024

Ulimwengu umeadhimisha leo Februari 06, siku ya kimataifa ya kupinga ukeketaji. Huko Tanzania wadau wa jinsia wamepaza sauti kukemea mbinu inayotumiwa na wanaoendekeza mila hiyo ya kuwakeketa watoto wakiwa wachanga.

https://p.dw.com/p/4c5S1
Ngariba wa zamani huko nchini Uganda
Mangariba hutumia nyembe na visu kuwafanyia tohara wanawake. Pichani ni Monica Cheptilak, aliyewahi kuwa ngariba huko nchini Uganda. Picha: Sally Hayden/Sopa Images/Zuma Press/Imago

Katika taarifa iliyotolewa na Mtandao wa asasi 12 za kupinga ukeketaji nchini humo, wadau hao wamesema, licha ya jitihada zinazofanywa na serikali, mashirika na taasisi, bado mila hiyo kandamizi ya ukeketaji inaendelea.

Takwimu za Demografia ya Afya za mwaka 2015 zinaonyesha kuwa, asilimia 10 ya wanawake wenye umri wa kati ya miaka 15-49 wamekeketwa Tanzania wakati takwimu za mwaka 2022 zinaonyesha idadi hiyo imepungua kwa asilimia 2 tu ambapo kwa sasa ni asilimia 8 ya wanawake wa umri huo wamekeketwa.

Mtandao huo umesema, wakeketaji wanabuni mbinu mpya na sasa wanawakeketa watoto wachanga.

Ukeketaji waripotiwa kwenye mikoa ambayo kabla haukuwepo 

Maandamano ya kupinga ukeketaji nchini Sierra Leone
Kampeni za kupinga ukeketaji barani AfrikaPicha: Saidu Bah/AFP

Kwa mujibu wa wanamtandao huo, ukeketaji wa watoto wachanga, ni ukatili mbaya unaoanza kupoteza haki za watoto wa kike wakiwa na umri mdogo zaidi.

Takwimu za demografia ya afya za mwaka 2022 zimeonyesha kuwa mikoa inayoongoza kwa ukeketaji Tanzania ni Arusha,asilimia 43, Manyara (43), Mara asilimia 28 na Singida 20.

Hata hivyo wadau hao wamesema, kuna mikoa ambayo awali haikuwa na ukeketaji lakini takwimu mpya zinaonyesha kuanzia mwaka 2022 wameanza kufanya ukeketaji.

Siku ya Kupinga ukeketaji hufanyika  Februari 6 kila mwaka, ambapo Umoja wa Mataifa, uliitambua rasmi siku hii baada ya kuona athari za ukeketaji kwa watoto wake. Kauli mbiu kwa mwaka ni "Sauti yake Hatima yake; Wekeza kwa manusura kutokomeza Ukeketaji”