1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tuzo ya haki ya kuishi yapata washindi

22 Septemba 2016

Kundi la wanaharakati wa kujitolea wanaooka maisha ya raia wa Syria wanaokabiliwa na mashambulizi ya kila siku, wanaharakati kutoka Misri, Urusi na gazeti moja la Uturuki wametunukiwa tuzo ya mwaka ya haki ya kuishi.

https://p.dw.com/p/1K6lj
Svetlana Gannushkina
Mwanaharakati wa Urusi Svetlana Gannushkina, mmoja wa washindi wa tuzoPicha: picture-alliance/dpa

Washindi wa tuzo hiyo iliyozinduliwa mwaka 1980 ikiwa na lengo la kutambua na kuthamini michango ya watu na vikundi ambavyo vinajitolea kuokoa maisha ya watu, watagawana kiasi cha dola 350,000, ambao ni pamoja na kikundi cha kutetea haki za raia nchini Syria maarufu kama White Helmets, mwanaharakati Mozn Hassan na vuguvugu lake la wanawake la Nazra kutoka nchini Misri, mwanaharakati wa Urusi Svetlana Gannushkina pamoja na gazeti huru la Uturuki la Cumhuriyet.

Mkurugenzi wa wakfu wa tuzo hiyo ambaye ni mpwa wa mwanzilishi wa tuzo hiyo Ole von Uexkull, amesema tuzo ya mwaka huu imezingasia changamoto kuu zinazoukabili ulimwengu kwa sasa - zikiwemo vita, uhuru wa kujieleza, haki za wanawake na masaibu yanayowakumba wahamiaji.

Ägypten Mozn Hassan
Mozn Hassan mwanaharakati kutoka nchini MisriPicha: M. Mohie

Uexkull amesema kikundi cha kutetea haki za wanawake cha Nazra kimetambulikwa kwa kuongeza uelewa wa watu katika kutambua uhumimu wa usawa na haki za wanawake kutoka katika mazingira ambayo yalikuwa yanawafanya wanawake kuwa wahanga katika machafuko, ubaguzi na unyanyasaji

Pia inaelezwa kuwa kikundi hicho kimefanikiwa kuweka rekodi ya matukio ya ukiukwaji wa haki za binadamu na kuhamasisha hatua dhidi ya unyanyasaji wa kingono uliofanyika kwa wanawake walioshiriki maandamano mwaka 2011 nchini Misri.

Utetezi wa haki za wakimbizi watambuliwa

Gunnashkina mtetezi wa masuala ya wanawake kutoka Urusi, ambaye pia ni mtetezi wa haki za wakimbizi ametambuliwa kwa kazi ya kuhamasisha utekelezaji wa haki za binadamu kwa wakimbizi, watu waliolazimishwa kuyakimbia makazi yao na utulivu miongoni mwa makundi yenye tabaka tofauti.

Gazeti la Cumhuriyet limesifiwa kwa kuandika habari za uchunguzi bila uoga katika mazingira ya ukandamizaji, ukaguzi na vitisho vya kufungwa na kuuwawa. Mhariri mkuu wa zamani wa gazeti hilo Can Dundar, na mwakilishi wake wa ofisi ya mjini Ankara Erdem Gul walihukumiwa kifungo cha miaka mitano gerezani mwezi Mei kutokana na ripoti zao juu ya usafirishaji wa silaha kimagendo kwa waasi wa Syria.

Tuzo ya haki ya kuishi - au tuzo mbadala ya Nobel, inalenga kutambua juhudi ambazo mwanzilishi wake Mhisani Jakob von Uexkull, Msweden mwenye asili ya Ujerumani, alihisi zinapuuzwa na tuzo za amani za Nobel.

Mwandishi: Celina Mwakabwale/AP/DW English

Mhariri:Iddi Ssessanga