1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uandishi wa raia waleta mabadiliko ya kisiasa na demokrasia kwa Afrika.

Sekione Kitojo21 Oktoba 2007

Mtu yeyote mwenye simu ya mkononi anaweza kupiga simu katika kituo cha radio nchini Ghana hivi leo, kumtaka waziri katika serikali ya nchi hiyo kujieleza kuhusu ahadi alizotoa wakati wa uchaguzi.

https://p.dw.com/p/C7go

Hii ni njia ya kufungua zaidi mawasiliano na serikali katika njia ya kidemokrasia.

Mapinduzi haya ya mawasiliano yamevunja ukuta uliokuwapo hapo zamani ambapo taarifa rasmi za serikali zilikuwa zikitolewa kuptia vyombo vinavyodhibitiwa na serikali, vya radio na televisheni. Hali hii imeleta hali bora zaidi ya uwazi na uwajibikaji katika hatua za utawala, anamesema Aida Opuku-Mensah, mkurugenzi wa habari na teknolojia ya mawasiliano katika tume ya uchumi ya umoja wa mataifa kwa Afrika mjini Addis Ababa, Ethiopia.

Jukumu la uandishi wa raia kama njia mpya kwa ajili ya kuimarisha demokrasia katika mataifa ya dunia ya tatu ilijadiliwa katika semina iliyoitishwa siku ya Jumanne wiki iliyopita na mpango wa hali bora kwa watoto na mashirika ya kimataifa ya kutoa huduma za kiutu, wizara ya mambo ya kigeni ya Finland na umoja wa waandishi wa habari nchini Finland ,SJL.

Mkurugenzi wa mipango wa Finland Riitta Weiste amesema katika semina hiyo kuwa uandishi wa habari wa raia haujaletwa kwa majadiliano katika sera za maendeleo.

Leo hii tunajiuliza , ICT inatuhakikishia mafanikio uandishi wa raia, na ni changamoto gani zinakutikana katika kazi na sera za maendeleo ya serikali na asasi zisizokuwa za kiserikali? Tunawezaje kutumia nyenzo za uandishi wa raia kwa kupunguza umasikini na kuchangia katika demokrasia.

Uandishi wa raia ni aina mpya ya wazo la zamani kuwa kunapaswa kuwa na maingiliano tofauti baina ya watoa habari na wale wanaozipokea, amesema Heikki Heikkila, mhadhiri mwandamizi katika idara ya uandishi wa habari na mawasiliano ya umma katika chuo kikuu cha Tampere nchini Finland. Hakupaswi kuwapo tu na uhuru wa kujieleza lakini pia uhuru wa kushiriki.

Katika mataifa yaliyoendelea kukiwa na nafasi kubwa ya mtandao wa internet, uandishi wa raia unatumika zaidi katika shughuli kama vile za blog na usambazaji wa maudhui kupitia tovuti zilizoanzishwa na watu binafsi.

Uandishi huu umewezekana kupitia maendeleo mapya ya teknolojia ya mawasiliano ambayo yamefanya uchapishaji kuwa rahisi na usio na gharama.

Uandishi wa raia umezuka kwa kiasi kikubwa kutokana na haja ya uandishi kuboresha utendaji wake wa kazi kulingana na utambuzi kuwa ulikuwa umejitenga mno na watu na maisha ya kawaida ya kila siku.

Kwa kujitoa kutoka katika utendaji wake wa zamani, gazeti la Time mwishoni mwa mwaka jana lilitoa tuzo yake ya kila mwaka ya mtu maarufu wa mwaka kwa watumiaji wa mtandao wa Internet.

Msingi wa tuzo hiyo ni kwamba watumiaji wa mtandao wa internet wameongezeka kwa kiasi kikubwa katika muda wa mwaka mmoja uliopita, hususan wanaotembelea katika tovuti mbali mbali ambapo watu wanaweza kushiriki kwa kuandika binafsi ama kuweka picha.

Katika mataifa ya Afrika hata hivyo, uandishi wa raia bado unafanyika kwa kiasi kikubwa katika maudhui ya matangazo ya radio, yanatumika kwa kiasi kikubwa, amesema Opuku-Mensah.