1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ufaransa mwenyeji wa mkutano wa mataifa ya Mediterania

Sekione Kitojo
10 Septemba 2020

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron atakuwa mwenyeji wa viongozi wa mataifa yanayopakana na bahari ya Mediterania kwa mkutano unapapangwa kuzungumzia hali ya wasi wasi kati ya Uturuki na mataifa ya mashariki mwa bahari hiyo

https://p.dw.com/p/3iFRY
Libanon Beirut Pressekonferenz Emmanuel Macron
Picha: picture-alliance/AP Images/G. Fuentes

Kundi  la  EuroMed7 ni kundi  ambalo si rasmi la  mataifa  saba  ya Umoja  wa  Ulaya  yanayopakana  na  bahari  ya  Mediterania, baadhi  ya  nyakati  yakijulikana  kama " klabu ya Med",  ambayo yalifanya  mara  ya  kwanza  mkutano  wao mwaka  2016 na ambayo  hayaijumishi  Uturuki.

Karte Korsika Haverie EN
Mkutano wa EuroMed7 utafanyika Corsica

Lakini mkutano huo  katika  kisiwa  cha  Ufaransa  cha  Corsica kitawaleta  pamoja  viongozi wa  Ufaransa, Italia, malta, Ureno na Uhispania pamoja  na  wanachama wa Umoja  wa  Ulaya  wa mataifa  ya  mashariki  mwa  bahari ya Mediterania Ugiriki  na Cyprus.

Ufaransa imeiunga  mkono  kwa  nguvu  Ugiriki  na  Cyprus  katika mkwamo  unaoongezeka  pamoja na  Uturuki kuhusiana  na  maliasili ya  gesi  na  mafuta  pamoja  na  ushawishi  wa  jeshi  la  majini katika  eneo  la  mashariki  mwa  Mediterania ambao umezusha  hofu za mzozo.

Mkutano  huo  utafanyika  leo mchana  katika  mji  wa  pwani  wa kitalii  nje  kidogo  ya  mji  mkuu  wa  jimbo  la  Corsica, Ajaccio.

Lengo  la  mazungumzo  hayo  ni  "kupiga  hatua  katika  kupata muafaka  juu  ya  uhusiano  wa  Umoja  wa  Ulaya  na  Uturuki  ikiwa pamoja  na  yote  kabla ya  mkutano  wa  Septemba  24-25 wa Umoja  wa  Ulaya,"  afisa  wa  ofisi  ya  rais  wa  Ufaransa amesema.

Mshirika muhimu

Akisisitiza sera ya  Macron kuelekea  Uturuki, afisa  huyo  alisema kuwa  Ufaransa inataka "ufafanuzi " katika  uhusiano  na  Ankara ambayo  inapaswa kuwa "mshirika  muhimu."

Uturuki imetaka  kujiunga  na  Umoja  wa  Ulaya  kwa   zaidi  ya  nusu karne  sasa na  wakati  juhudi  zake  za  kuwa  mwanachama zimekwama vibaya  katika  miaka  michache  iliyopita, na  haionekani tena  kuwezekana katika  baadhi  ya  sehemu, inabaki kuwa mgombea  wa  kujiunga  na  kundi  hilo  la  mataifa.

Utafutaji  wa  Uturuki  wa  gesi  na  mafuta  katika  eneo  la  maji linalodaiwa  na  Ugiriki kuwa  ni  lake  umeathiri  pa kubwa  uhusiano kati ya  mataifga  hayo  mawili  wanachama  wa  NATO.

Türkei Das seismisches Forschungsschiff Oruc Reis bei Istanbul
Meli ya utafutaji mafuta na gesi ya Uturuki Oruc ReisPicha: Reuters/Y. Isik

Uturuki  mwezi  uliopita  iliweka vyombo  vya  utafutaji  wa  mafuta na  gesi , meli  ya  Oruc Reis  katika  eneo  la  maji  kati  ya  Ugiriki na  Cyprus, hali  iliyosababisha  Ugiriki  kufanya  mazowezi ya kijeshi baharini.

Baadhi  ya  mataifa  wanachama  yatataka  kuiwekea  vikwazo Uturuki  katika  mkutano  wa  kilele wa  Umoja  wa  Ulaya, ambapo waziri  wa  mambo  ya  kigeni  wa  Ufaransa  Jean-Yves Le Drian alisema  mwishoni  mwa  juma  hatua  kama  hizo  ziko  mezani.