1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani kuisaidia Afrika Mashariki kupambana na corona

Lilian Mtono
30 Machi 2020

Serikali ya Ujerumani imesema itatoa msaada wa vifaa tiba pamoja na kiasi cha fedha taslimu kwa mataifa ya Afrika mashariki, katika jitihada za kuongeza nguvu ya mapambano dhidi ya virusi vya Corona. 

https://p.dw.com/p/3aDEb
Logo Ostafrikanische Gemeinschaft EAC

Ingawa mataifa yote sita ya Afrika Mashariki yameendelea kuchukua hatua ili kuhakikisha maambukizi ya homa kali ya mapafu inayosababishwa na kirusi cha corona havienei zaidi na kuleta madhara kwa wakaazi wa eneo hilo llililo kusini mwa jangwa la sahara, juhudi zaidi zinahitajika kudhibiti ugonjwa huo ambao umesababisha madhara makubwa kwa mataifa ya ulimwengu.

Katika kuunga mkono jitihada hizi serikali ya Ujerumani katika mpango wake maalum na waharaka inataraji kukabidhi maabara zinazohamishika kwa kila taifa la Afrika Mashariki ambazo zitakuwa na uwezo wa kugundua magonjwa mbalimbali ikiwemo virusi vya covid-19

Balozi wa ujerumani nchini Tanzania Regine Hess amesema, kiasi cha Euro milioni moja na nusu zitatumiwa katika kukamilisha mpango huo, ambapo kila taifa litapokea maabara zinazohamishika mbili huku kwa upande wa serikali ya Tanzania kadhalika itanufaika na vifaa elfu moja vya kubaini virusi vya covid-19.

Tansania | Deutsche Botschafterin Regine Hess
Balozi wa Ujerumani nchini Tanzania Regine Hess.Picha: DW/H. Bihoga

Msaada huo wa serikali ya Ujerumani kwa mataifa ya Afrika Mashariki umetajwa kuelekeza nguvu zaidi katika mipaka ikiwemo pia viwanja vya ndege, mafunzo kwa wahudumu wa afya katika maeneo hayo kadhalika msaada wa kiufundi.

Katika ushauri wake wa kusisitiza watu katika jumuia ya Afrika Mashariki kuchukua tahadhari dhidi ya maammbukizi hatari za corona balozi Hess, amesema kuna umuhimu wa kuzingatia tahadhari zote zinazotolewa na wataalamu wa afya ili kuwa salama na maambukizi hayo hatari yaliogharimu maisha ya watu zaidi ya watu elfu  34 kote ulimwenguni.

Hata hivyo wachambuzi wa masuala ya kidiplomasia bado wanasisitiza kwa nchi za jumuia ya Afrika mashariki kuwa kuna haja ya kuunganisha jitihada zao katika mapambano haya, kutokana na wananchi wake kuwa na muingiliano mkubwa kijamii, kiutamaduni na hata kiuchumi.

Mwandishi: Hawa Bihoga Dw Dar es salaam