1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMarekani

Urusi: Marekani imeamua kuzidisha mzozo nchini Ukraine

Lilian Mtono
27 Januari 2023

Urusi imesema Marekani ilikuwa na uwezo mkubwa wa kuumaliza mzozo unaosidi nchini Ukraine, lakini badala yake iliamua kuchukua hatua za kuuchochea zaidi.

https://p.dw.com/p/4Mnbl
Präsident Joe Biden zu Ukraine-Hilfe
Picha: Susan Walsh/AP/picture alliance

Urusi imesema leo kwamba Rais Joe Biden wa Marekani ana uwezo mkubwa wa kuumaliza mara moja mzozo unaoendelea nchini Ukraine, lakini badala yake ameamua kuchagua njia ya kuuzidisha kwa kuendelea kuipatia silaha nchi hiyo. Amesema hayo, wakati Umoja wa Ulaya ukitoa mwito wa Urusi kuwajibishwa kutokana na uhalifu mkubwa ilioufanya nchini Ukraine. 

Msemaji wa ikulu ya Kremlin Dmitry Peskov amesema mapema leo kwamba rais Biden ana nafasi kubwa ya kuvimaliza vita vya nchini Ukraine, tena mara moja. Peskov amewaambia waandishi wa habari kwamba Biden hakutaka kuchagua njia hiyo na badala yake ameamua kuendelea kuijaza silaha Ukraine. 

Soma Zaidi:Marekani kuipelekea Ukraine vifaru chapa M1 Abrams 

"Wasiwasi unazidi kuongezeka... miongoni mwa mengineyo ni maamuzi yaliyochukuliwa mara ya kwanza na yaliyoendelea kuchukuliwa na Washington na mataifa ya Ulaya kwa shinikizo la Washington. Kuipa Ukraine silaha, vifaru na vingine, mwendelezo wa majadiliano juu ya kuipa vifaa vya angani na kadhalika...kwa ujumla haya yanazidisha mvutano," amesema Peskov.

Ulaya yataka mahakama ya kimataifa kuishitaki Urusi.

Katika hatua nyingine, mawaziri wa sheria wa Umoja wa Ulaya wanataka Urusi iwajibishwe mara moja kutokana na uhalifu waliouita wa kutisha nchini Ukraine, licha ya kutofautiana kuhusu mbinu za kutumika katika mjadala kuhusu jinsi Urusi inavyoweza ya kufunguliwa mashtaka, mchakato wa kutafuta ushahidi pamoja na kufadhili ukarabati wa nchi hiyo iliyoharibiwa na vita.

Ukraine | Zerstörung in der Stadt Hlevakha
Moja ya majengo yaliyoharibiwa vibaya kufuatia mashambulizi yaliyofanywa na Urusi nchini Ukraine. Inakaribia mwaka mmoja tangu kwa mara ya kwanza Urusi ilipolivamia taifa hilo jirani.Picha: Valentyn Ogirenko/REUTERS

Mawaziri hao 27 wamekutana mjini Stockholm kuelekea maadhimisho ya mwaka mmoja tangu Urusi ilipoivamia kikamilifu Ukraine, Februari 24. Waziri wa sheria wa Iceland Simon Harris, amesema kuna umuhimu mkubwa wa Urusi kuwajibishwa kwa uhalifu wa kutisha na ukatili unaoushuhudiwa nchini Ukraine, kwa kuangazia namna bora zaidi za kupata ushahidi pamoja na kuundwa mahakama mpya ya uhalifu ili kuishitaki.

Nchini Ukraine, mamlaka zimeripoti mapigano makali dhidi ya wanajeshi wa Urusi wanaojaribu kujipenyeza katika eneo la mashariki na kaskazinimashariki mwa nchi hiyo, kabla Kyiv haijafikiwa na vifaru ilivyopewa na washirika wa magharibi, na kusema hali hiyo inaashiria kwamba wanahitaji silaha zaidi ili kuwadhibiti wavamizi.

Kyiv imesema mapigano hayo makali yaliyokuwa yakiendelea, siku moja baada ya karibu watu 11 kuuawa katika mashambulizi ya makombora na ndege zisizo na rubani yanazingatiwa na Ukraine kama jibu la ahadi za washirika wake za kuipatia vifaru vya kisasa zaidi.

Soma Zaidi: Ukraine kupokea magari zaidi ya kivita