1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Utawala wa rais Barack Obama kujenga uhusiano na mataifa ya Kiarabu.

Eric Kalume Ponda/Afp27 Januari 2009

Rais wa Marekani, Barack Obama, sasa ameanza kuelekeza juhudi zake kuujenga na kuimarisha uhusiano baina ya Marekani na mataifa ya Kiarabu.

https://p.dw.com/p/Gh3W
Rais Barack Obama wa MarekaniPicha: AP

Na ili kufikia hilo, Rais Obama amesema ipo haja ya kuendelea na mazungumza na mataifa ya kiarabu, ikiwemo Iran ambayo uhusiano wake na Marekani umezorota kufuatia mpango wake wa Nuklia, huku Mjumbe maalum wa Marekani katika eneo la Mashariki ya kati, George Mitchell, akianza ziara yake kusukuma ajenda ya Marekani katika kutafuta amani ya eneo hilo.


Akisema kuwa Marekani sio adui wa mataifa ya Kiarabu, Rais Barack Obama hakusita kueleza njia ndefu ya maisha yake katika kusisitiza dhamira yake ya kuleta uhusiano baina ya Marekani na mataifa hayo ya Kiarabu.

Akizungumza kwa mara ya kwanza, kupitia televisheni ya kiarabu ya Al Arabiya, Rais Obama alisema yeye, kama Mtu aliyelelewa nchini Indonesia kwa miaka mingi, na kuzuru mataifa mengi ya kiarabu wakati wa utoto wake, na bila ya kujali misingi ya kidini, hana shaka lengo lake la kuleta uhusiano baina ya Marekani na mataifa ya Kiarabu litafikiwa.

Rais Barack Obama alisema kuwa Historia ya Marekani haionyeshi kuwa ni taifa lenye kutaka kutawala mataifa mengine, na kwamba hakuna sababu kumzuia kufikia lengo hilo.

Hivyo basi alisema kuwa hivi karibuni atatembelea baadhi ya mataifa ya Kiarabu na kufanya mashauriano na Iran ili kufikia suluhisho la amani kuhusiana na suala la mpango wake wa Nuklia.

Hali kadhalika, alisema kuwa dhamira yake kubwa ni kuona amani ikidumishwa katika eneo la mashariki ya kati.

Hivyo basi Mjumbe maalum wa Marekani katika eneo hilo, George Mitchelle, ameanza ziara yake katika eneo hilo akiwa na ujumbe maalum kutoka kwa Rais Barack Obama.

Mjumbe huyo anatarajiwa kuzuru Israel, Palestina, Jordan na Saudi Arabia ili kutoa msukumo zaidi wa kupatikana amani ya kudumu kufuatia vita baina ya Israel na Wafuasi wa chama cha Hamas. Mjumbe huyo anatarajiwa kumuarifu Rais Obama na waziri wa mambo ya nchi za Nje, Hillary Clinton, ili kuweza kubuni maongozi yaafayo.

Wakati huo huo, Rais Barack Obama leo alifanya mashauri ya kina na wabunge wa chama cha Republican kuhusiana na mpango wake wa dola bilioni 800 kuokoa uchumi wa taifa hilo.

Kumekuweko tofauti kubwa baina ya wabunge wa chama cha Democrat na wale wa Republican kuhusiana na mpango huo ambao unaonekana kupingwa vikali na wabunge wa Republican ambao wanasisitiza kwamba masharti yao ya kupunguzwa kiwango cha kodi na matumizi hayajakubaliwa.

John McCain im Ryman Auditorium in Nashville
John McCain wa chama cha RepublicanPicha: AP

Miongoni mwa wale ambao wamesema kuwa wanaupinga mpango huo ni pamoja na aliyekuwa mpinzani wa Rais Barack Obama wakati wa kampeni za uchaguzi, Seneta John McCain.

Bunge hilo linatarajiwa kuupigia kura mpango huo hapo kesho, huku Rais Obama akisema kuwa nia yake ni kusaini mswada huo kuwa sheria kabla ya Februari 16.