1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waandishi riwaya wa Afrika wamulikwa Berlin

Mohmed Dahman3 Oktoba 2008

Usomaji,midahalo ya fasihi na matukio ya muziki yenye kulenga fasihi ya Kiafrika imewakusanya pamoja madarzeni ya waandishi riwaya,washairi na wanamuziki mjini Berlin kwa Tamasha la Fasihi la Kimataifa la Berlin.

https://p.dw.com/p/FTMD
Fatou Diome wa Senegal ni mmoja wa waandishi riwaya mashuhuri kutoka Afrika waliohudhuria Tamasha la Fasihi la Kimataifa la Berlin.Picha: dpa

Majina mashuhuri ya Afrika kama vile mwandishi riwaya mkongwe mzalia wa Somalia Nuruddin Farah,Fatou Diome wa Senegal,Lebogang Mashile wa Afrika Kusini na Helon Habila wa Nigeria ni baadhi tu ya vigogo wa fasihi waliohudhuria tamasha hilo la siku 11.

Vitabu vya riwaya vya Farah na michezo ya kuigizwa majukwaani na kwenye radio kwa miaka mingi vimekuwa vikitafsiriwa katika lugha zaidi ya 20.Mara nyingi mwandishi huyo wa riwaya amekuwa akilenga hadithi zake juu ya hali ya wanawake baada ya kipindi cha ukoloni nchini Somalia hususan katika dhana ya kupoteza utambulisho wa taifa.

Ulrich Schreiber mtayarishaji wa tamasha hilo anasema wana furaha kwamba mwanariwaya huyo ameweza kuwa pamoja nao akionekana kuwa na shajaa kwa kushiriki kwa waandishi wenye kipaji wa Afrika.Siku hizi Farah anaishi Cape Town nchini Afrika Kusini.

Mbunge wa Kenya na mwandishi wa riwaya Joseph Lemasolai Lekuton ambaye fasihi yake juu ya maisha ya mtu ambacho kilikuwa ni kitabu chake cha kwanza Facing The Lion (Kumkabili Simba) kilichojipatia sifa barani Afrika ametumia tamasha hilo kuwaelezea watu waliohudhuria mjini Berlin juu ya uzoefu wake wa maisha ya utotoni akikulia kaskazini mwa Kenya na kwamba kabila lake ni la Wamasai.

Lekuton ambaye ana kaka watatu na dada mmoja anasema kufa kwa vituo vya elimu katika mkoa aliokuwa akiishi kulimaanisha kwamba alikuwa ni mtu pekee katika familia yake aliyeweza kuhudhuria shule.Hapo mwaka 1989 wakati alipopata nafasi ya kusoma Marekani kijiji chake kiliuza n'gombe kadhaa kusaidia kugharamia safari yake.

Akiwa ni mbunge tokea mwaka 2006 Lekuton amesema hivi sasa anajituma mwenyewe kuboresha mfumo wa elimu wa taifa na miundo mbinu vijijijni.

Ingawa kwa jumla anaweka hali ya Kenya kuwa mbaya Lekuton anakiri kwamba maendeleo fulani yamefikiwa katika kipindi cha nusu karne iliopita.Anasema vijana wengi wadogo wanakwenda shule na vyuo vikuu vingi vinajengwa.

Hata hivyo Lekuton anasisitiza kwamba Kenya bado ingali inahitaji kuodokana na mizozo ya kikabila na wivu na kushughulikia ugawaji wa ardhi utakaozingatia haki ili kuepuka ghasia zaidi za umwagaji damu.

Mwandishi mzalia wa Ghana Amma Darko pia amefurahia kutangazwa sana katika tamasha hilo. Mwanamke huyo alianza kutunga riwaya yake ya kwanza Beyond the Horizon(Kupindukia Upeo wa Macho) baada ya kuhamia Ujerumani hapo mwaka 1981 akikimbia kutokuwepo kwa utulivu wa kisiasa huko nyumbani.Kufikia wakati kitabu hicho kilipochapishwa ikiwa ni muongo mmoja baadae nchini Ujerumani alikuwa hayupo tena kuweza kukishuhudia kutokana na kuwa kesharudi nyumbani.

Kitabu hicho juu ya hatima ya kijana mmoja wa kike wa Ghana ambaye amemfuata mume wake nchini Ujerumani na baadae kulazimishwa kuingia kwenye ukahaba kinaelezea dhana zisizo sahihi walizonazo Waafrika wengi juu ya Ulaya na hofu walio nayo ya kuwakatisha tamaa watu waliowawacha nyuma huko Afrika.

Tokea wakati huo Darko ambaye ameolewa na ana watoto watatu ametunga vitabu kadhaa vya riwaya cha karibuni kabisa kikiwa ni Smile of Nemesis chenye kuelezea tamaa,kutoamini dini na kuowa wake wengi nchini Ghana ambapo pia anafanya kazi kama mkaguzi wa kodi mjini Accra.

Tamasha hilo litafungwa Jumapili kwa tukio la kumtukuza mwandishi aliependwa mno wa Kipalestina marehemu Mahmoud Darwish aliefariki nchini Marekani mwezi uliopita baada ya kufanyiwa operesheni ya moyo.