1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wakenya walia na bei mpya za petroli na dizeli

Sylvia Mwehozi
16 Septemba 2023

Mamlaka ya udhibiti wa nishati na Petroli nchini Kenya, imetangaza kupanda kwa bei za mafuta na kufikia rekodi ya juu na kuongeza maumivu kwa mamilioni ya Wakenya wanaokabiliwa na kupanda kwa gharama za maisha..

https://p.dw.com/p/4WPSf
Kenia Kleinbusse Matatu
Picha: Getty Images/AFP/T. Karumba

Kulingana na tangazo la mamlaka hiyo, bei ya reja reja ya lita moja ya mafuta ya petroli imepindukia shilingi 200 za Kenya sawa na dola 1.36 za Kimarekani, bei ambazo hazijawahi kushuhudiwa.

Chini ya bei hizo ambazo zimeanza kutumika tangu Ijumaa na zitadumu hadi Oktoba 14, lita moja ya petroli katika mji mkuu wa Nairobi imepanda kwa takriban shilingi 17 na itauzwa kwa shilingi 211.64 na dizeli ni shilingi 200.99.

Ongezeko la bei za mafuta 2022: Kenya: Mafuta na petroli zapanda bei kwa shilingi 20

Wakenya tayari wanakabiliwa na hali mbaya ya gharama za juu za maisha kutokana na kupanda kwa bei ya bidhaa nyingi za msingi, msururu wa kodi mpya na kuporomoka kwa thamani ya shilingi.

Kenya
Maandamano ya Kenya mwezi JulaiPicha: Thomas Mukoya/REUTERS

Ripoti za vyombo vya habari vya Kenya zinasema kuwa nauli za matatu yani mabasi madogo yanayotumiwa na Wakenya walio wengi, pia zinatarajiwa kupandishwa huku Chama cha Wamiliki wa Matatu kikitangaza ongezeko la asilimia 20 kote nchini.

Upinzani nchini Kenya umefanya maandamano kadha dhidi ya serikali ya Rais William Rutona sera zake za kiuchumi. Mawaziri wa serikali wamelaumu kwa kiasi fulani kupunguzwa kwa uzalishaji wa mafuta kulikotangazwa mapema mwezi huu na wazalishaji wakuu Saudi Arabia na Urusi ambako kumesababisha bei ya mafuta ghafi duniani kupanda. 

Waziri wa nishati wa Kenya Davis Chirchir aliieleza kamati ya nishati ya bunge kwamba "hakuna chochote tunachoweza kufanya, hakika maumivu ni makubwa, haitakuwa rahisi." Naye waziri wa biashara na viwanda Moses Kuria alionya kupitia mtandao wa X, kwamba Wakenya watarajie bei ya mafuta kupanda kwa shilingi 10 kila mwezi hadi Februari.Mkwamo wa kisiasa Kenya kutatuliwa?

Kenya
Mwandamanaji na bango lenye ujumbePicha: Samson Otieno/AP/picture alliance

Bei ya mafuta imekuwa ikiongezeka kutokana na kuondolewa kwa ruzuku kulingana na matakwa ya Shirika la Fedha duniani IMF na kuongezeka maradufu kwa kodi ya mapato VAT katika bidhaa za mafuta kwenye Sheria ya Fedhaambayo haikupokolewa vyema na umma na ilitiwa saini na rais Ruto kuwa sheriamnamo mwezi Juni. 

Sheria hiyo inatoa mwanya wa kuanzishwa kodi nyingi mpya na zilizoongezwa ambazo serikali inasema zinahitajika ili kuboresha fedha za umma na kupunguza mzigo wa deni la taifa. Mahakama ya Nairobi inatarajiwa kutoa uamuzi mwezi Novemba kuhusu pingamizi la kisheria dhidi ya Sheria ya Fedha na walalamikaji wanaosema ni kinyume cha katiba.

Ripoti za vyombo vya habari zinasema serikali inazingatia kuongezea kodi zaidi ikiwa ni pamoja na kuongeza VAT na ushuru unaolenga wakulima na wamiliki wa magari miongoni mwa wengine, kulingana na mkakati wa mapitio wa wizara ya fedha wa mwaka 2026/27.

Wakenya wengi wamemshutumu Ruto kwa kuvunja ahadi alizotoa kwenye kampeni za uchaguzi wa mwaka jana, alipoahidi kuboresha maisha ya watu wa kawaida.