1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroMali

Watoto milioni 1.8 wamekimbia makaazi yao ukanda wa Sahel

22 Machi 2024

Save the Children imesema watoto milioni 1.8 wamelazimika kuyakimbia makaazi yao kufuatia kuongezeka kwa ghasia nchini Mali, Burkina Faso na Niger, idadi hiyo ikiwa ni ongezeko la mara tano katika muda wa miaka mitano.

https://p.dw.com/p/4e04Q
Watu waliokimbia makaazi yao kutoka jimbo la Cabo Delgado wamekusanyika kupokea msaada kutoka kwa Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP)
Watu waliokimbia makaazi yao kutoka jimbo la Cabo Delgado wamekusanyika kupokea msaada kutoka kwa Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP)Picha: ALFREDO ZUNIGA/AFP/Getty Images

Mkurugenzi wa uendeshaji miradi kanda ya Afrika Magharibi na Kati wa Save the Children Vishna Shah, ameutaja mzozo uliosahaulika katika eneo la Sahel kuwa moja kati ya majanga makubwa zaidi ya kibinadamu duniani.

Shirika hilo la hisani limejumuisha idadi ya watoto waliokimbia makaazi yao katika nchi tatu za eneo la Sahel kwa kutumia takwimu zilizotolewa na Kamishna Mkuu wa shirika la kuhudumia wakimbizi UNHCR na shirika la kimataifa la uhamiaji IOM.

Soma pia: UN: Mwaka 2023 ulikuwa mbaya kwa wahamiaji 

Takwimu zinaonyesha kuwa idadi ya watoto waliolazimika kuyakimbia makazi yao imeongezeka kutoka karibu 321,000 mnamo mwaka 2019 na kufikia milioni 1.8 mwaka huu.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, watoto wanawakilisha asilimia 40 ya watu waliokimbia maakazi yao duniani kote japo idadi hiyo ni kubwa zaidi kanda ya Afrika Magharibi na Kati.