1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

WHO: Mapambano ya COVID-19 yatakuwa magumu

Yusra Buwayhid
7 Januari 2021

Wataalamu wa Shirika la Afya Duniani wameonya kwamba miezi sita ijayo ya 2021 itakuwa migumu kabla ya chanjo dhidi ya ugonjwa wa COVID-19 kuanza kutoa kinga na kuleta afueni wakati wa janga hili la virusi vya corona.

https://p.dw.com/p/3ncwg
USA Coronavirus Impfstoff-Test
Picha: H. Pennink/AP Photo/picture-alliance

Maria Van Kerkhove, kiongozi wa kiufundi wa WHO katika kitengo cha kupambana na Covid-19, amesema katika nchi nyingi hasa kwenye bara la Ulaya na eneo la Amerika Kaskazini, hali inayoshuhudiwa ni ya kutia wasiwasi sana - na inatarajiwa kuwa mbaya zaidi siku za usoni.

"Nchi kadhaa zinapambana na idadi kubwa ya maambukizi," haswa Ulaya na Amerika Kaskazini, na "kunashuhudiwa idadi ya kutisha sana ya wagonjwa kulazwa hospitalini na katika vitengo vya wagonjwa mahututi", alisema Van Kerkhove.

Ameongeza kwamba hali hiyo imetokana na watu kutembeleana sana majumbani kipindi cha sherehe za Krismasi na mwaka mpya. Na hivyo mtaalamu huyo wa WHO ametahadharisha kuwa idadi ya maambukizi ya virusi vya corona itaongezeka Januari.

Naye Michael Ryan, mkurugenzi wa nyakati za dharura wa WHO amesema, kulikuwa na matarajio makubwa wakati chanjo zilipoanza kutiririka mwezi uliopita, lakini hilo halimaanishi kuwa watu waanze kujisahau na kuacha kuwa waangalifu dhidi ya ugonjwa huo.

Soma zaidi: Chanjo zaanza kutolewa katika Umoja wa Ulaya

Amesisitiza kwamba miezi mitatu hadi sita ijayo, ulimwengu utakabiliwa na kibarua kigumu cha mapambano dhidi ya virusi vya corona lakini mafanikio yatapatikana.

Wakati huo huo, Umoja wa Ulaya umeidhinisha chanjo ya pili dhidi ya virusi vya corona iliyotengenezwa na kampuni ya Marekani Moderna kutumika barani humo.

Schweiz Genf | Maria van Kerkhove, WHO
Maria van Kerkhove, kiongozi wa kiufundi wa WHOPicha: picture-alliance/dpa/Keystone/F. Coffrini

Lakini pia mchakato wa kusambaza dozi ya kwanza ya chanjo kati ya mbili zinazohitajika bado unazorota, huku virusi hivyo vikiendelea kusababisha idadi kubwa ya vifo ulimwenguni kote.

Idadi ya chanjo dhidi ya COVID-19 yaongezeka

Hapa Ujerumani gazeti la Bild limeripoti kwamba kampuni ya madawa ya CureVac imekubali kushirikiana na nyingine ya Bayer kutafuta msaada wa kimataifa, ili chanjo yao mpya inayofanyiwa majaribio iweze kuidhinishwa na kusabazwa.

Kwa upande wa Uingereza, baadhi ya madaktari wameruhusiwa kuanza kutoa chanjo Thursday iliyotengenezwa nchini humo kwa ushirikiano wa kampuni ya madawa ya AstraZeneca na Chuo Kikuu cha Oxford nchini humo.

Kwengineko ulimwenguni, katika jimbo la Heibei huko China kumeripotiwa ongezeko kubwa la maambukizi ya COVID-19 ndani ya siku moja. Mamlaka husika zimetangaza masharti magumu zaidi ya kujikinga na maambukizi hayo. Wakati huo huo Japan imetangaza hali ya dharura ya mwezi mzima katika mji wake mkuu wa Tokyo pamoja na maeneo mengine matatu jirani na mji mji huo.

Aidha barani Afrika, Tunisia imetangaza maambukizi mapya ya wagonjwa wapatao 2,820 ikiwa ni idadi kubwa zaidi tangu kuzuka janga la virusi vya corona. Na Morocco nayo iimeamua kuiunga mkono Uingereza na kuidhinisha utumiaji wa chanjo iliyotengenezwa na kampuni ya AstraZeneca na Chuo Kikuu cha Oxford nchini humo.

(afp,rtre)