1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Zelensky:Muhimu ni vifaru chapa Leopard

21 Januari 2023

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amesema hakukuwa na njia mbadala kwa nchi za Magharibi bali kuipa Ukraine silaha nzito, huku Ujerumani ikishindwa kuthibitisha iwapo itatoa vifaru vyake chapa Leopards

https://p.dw.com/p/4MWmN
Deutschland Ramstein Air Base | Beratungen über Militärhilfe für Ukraine | Pistorius & Austin & Resnikow
Picha: Andre Pain/AFP/Getty Images

Mkutano ulioongozwa na Marekani uliwahusisha washirika takriban 50 wa Ukraine, umepitisha msaada wa kijeshi wenye thamani wa mabilioni ya dola, ikiwa ni pamoja na magari ya kivita na silaha zinazohitajika kurudisha nyuma vikosi vya Urusi kwenye uwanja wa mapambano.

Hata hivyo rais Zelensky katika mkutano huo amesisitiza anahitaji zaidi vifaru vya kivita juu ya msaada huo uliopitishwa kwa taifa lake.

Akihutubia mkutano huo kwa njia ya video, Zelensky aliwahimiza washirika hao "kuharakisha" upelekwaji wa silaha na kuweka mkazo upatikanaji ya vifaru chapa Leopard 2, kutoka Ujerumani.

"Kila siku tunaona kwamba hakuna mbadala, zaidi ya kufanya maamuzi kuhusu upatikanaji wa vifaru" Alisema Zelensky katika hotuba yake.

Soma Pia:Ujerumani: Bado hakuna mwafaka wa kupeleka vifaru Ukraine

Matarajio yaliongezeka kwa washirika wa Kyiv, kabla ya mkutano wa siku ya Ijumaa uliongezwa na Austin, kwamba Ujerumani ingelikubali walau nchi zingine zinazotumia aina hiyo ya vifaru aina ya Leopard, wangeruhusiwa kuvipeleka Ukraine.

Sababu za Ujerumani kusita kutoa majibu ya moja kwa moja bado hazijawa wazi, kwani Uingereza imekubali kutuma vifaru vyake 14 aina ya Challenger 2 nchini Ukraine.

Ujerumani: Berlin ni mshirika muhimu wa Kyiv

Waziri wa Ulinzi wa Marekani Lloyd Austin alisema Ukraine inatarajiwa kufanya mashambulizi dhidi ya vikosi vya Urusi katika wiki zijazo.

Ramstein-Treffen zum Krieg in der Ukraine | Verteidigungsminister Pistorius
Waziri wa ulinzi Ujerumani Boris PistoriusPicha: dpa

"Tunayo fursa kwa sasa na majira ya masika, wakati wowote watapoanza mashambulizi yao" Alisema waziri wa ulinzi Marekani, akiwa katika mkutano uliofanyika katika kambi ya jeshi ya anga ya Ramstein Ujerumani.

Waziri waUlinzi wa Ujerumani Boris Pistorius aliwaambiawaandishi wa habari- "Bado hatuwezi kusema ni lini uamuzi utachukuliwa, na uamuzi utakuwa upi, linapokuja suala la vifaru vya chapa Leopard."

Austin aliitetea Ujerumani dhidi ya ukosoaji kwamba haikuwa ikifanya vya kutosha kuisaidia Kyiv, akisema serikali yake imekuwa mshirika wa kutegemewa na Ukraine.

"Sote tunaweza kufanya zaidi," Alisema Austin, akisisitiza kwamba Berlin ilikuwa "mshirika wa kutegemewa".

Maafisa wa Marekani walisema Ukraine bado inakabiliwa na vita kali dhidi ya majeshi ya Urusi, ambayo bado yanashikilia moja ya tano ya nchi hiyo, ikiwa ni takriban miezi 11 sasa baada ya uvamizi wa Moscow.

Soma Pia:Ujerumani yazidi kushinikizwa kuisaidia Ukraine

Hata hivyo walizungumzia juu ya oparesheni ijayo ambayo wanataja kwamba Ukraine itarejesha sehemu ambazo Urusi inazidhibiti.

Jenerali Mark Milley ambae ni mkuu wa majeshi Marekani ameeleza kiwango cha vifaa vinavyohitaji, ikiwa ni pamoja na magari ya kijeshi,silaha pamoja na mafunzo kwa vikosi vya Ukraine ambayo Kyiv imekuwa ikiahidiwa.

Moscow yaonywa utolewaji vifaru chapa Leopard, Kyiv

Der russische Pressesprecher Dmitry Peskov
Msemaji wa Kremlin Dmitry PeskovPicha: Elena Palm/ZUMAPRESS.com/picture alliance

Siku ya Ijumaa Kremlin imeonya kwamba vifaru vya washirika wa magharibi kupelekwa Ukraine kutasababisha hali kuwa ngumu zaidi.

Katika mkutano wake na waandishi wa habari msemaji wa Kremlin Dmitry Peskov alisema, hoja hiyo haipaswi kupewa uzito mkubwa.

"Tunaona ufuasi wa udanganyifu mkubwa juu ya uwezekano wa Ukraine kuwa na mafanikio kwenye uwanja wa vita," Peskov Aliwaambia wanahabari.

Soma Pia:Bado hakuna makubaliano ya Ujerumani kupeleka vifaru Ukraine

Alionya kwamba utolewaji wa misaada hiyo utaongeza tatizo zaidi kwa Ukraine, lakini haitabadilisha kitu kwa vikosi vyake katika kusonga mbele kwenye uwanja wa vita,kufikia malengo yake.

"Hii itaongeza matatizo kwa Ukraine, lakini kwa upande wa Urusi haitabadili chochote katika kufikia malengo yake."

Kwenye Uwanja wa mapambano Bakhmut,Ukraine

Wizari wa Ulinzi Urusi imesema vikosi vyake vimechukua udhibiti wa eneo la Klishchiivka, ambayo ni makaazi ya kusini mwa mji wa Bakhmut katika eneo la kimkakati la Donesk Mashariki mwa Ukraine

Wiki iliyopita, vikosi vya Urusi vilitaja kuuteka mji wa Soledar kaskazini Mashariki mwa Bakhmut, hatua inayotajwa na wachambuzi wa masuala ya ulinzi kuwa inaweza kuwasaidia kuweka shinikizo kwa mji mkubwa.

Soma Pia:Marekani yawapa mafunzo askari wa Ukraine nchini Ujerumani

Mji huo uliokuwa na wakaazi 400 kabla ya vita, ulitekwa kwa msaada wa mashambulizi ya anga.

Hata hivyo taarifa hizo hazijathibitishwa na mamlaka ya Ukraine kutoka katika uwanja wa vita

Ukraine yaendelea kuyakomboa maeneo yake