1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa AU walenga kuimarisha sauti ya Afrika kimataifa

Iddi Ssessanga
15 Februari 2024

Mkutano wa kilele wa kila mwaka wa Umoja wa Afrika utafunguliwa siku ya Jumamosi wakati bara hilo likikabiliwa na jinamizi la mapinduzi na mizozo ya kisiasa, vinavyotatiza malengo yake ya kuimarisha uwepo wake kimataifa.

https://p.dw.com/p/4cRY4
Picha ya ishara| Umoja wa Afrika | Picha ya pamoja
Viongozi wakuu wa serikali a mataifa ya Afrika hukutana alau mara moja kila mwaka mjini Addis Ababa, Ethiopia.Picha: Amanuel Sileshi/AFP

Ikiundw azaidi ya miongo miwili iliyopita, jumuiya hiyo yenye wanachama 55 imekosolewa kwa muda mrefu kwa kukos ufanisi na kuchukua hatua kidogo sana yanapotokea mapinduzi.

Gabon na Niger hazitahudhuria mkutano huo katika mji mkuu wa Ethiopia, Addis Ababa, kufuatia kusimamishwa kwao kutokana na mapinduzi mwaka jana. Wataungana na Mali, Guinea, Sudan na Burkina Faso, ambazo pia zimezuiwa kushiriki katika mkutano huo.

Mapinduzi na mzozo nchini Senegal, ambayo imekumbwa na msukosuko tangu Rais Macky Sall kuahirisha uchaguzi wa mwezi huu katika dakika za mwisho, huenda ukatawala ajenda, alisema mchambuzi Nina Wilen.

"Nina shaka kwamba kutakuwa na maamuzi yoyote yenye nguvu," Wilen, mkurugenzi wa programu ya Afrika katika Taasisi ya Uhusiano wa Kimataifa ya Egmont mjini Brussels alisema.

Shirika hilo hadi sasa lina "ushawishi mdogo sana kwa nchi ambazo zimekumbwa na mapinduzi ya hivi karibuni", alisema, akiongeza kuwa nchi wanachama hazikutaka kuweka mifano ambayo inaweza kugongana na maslahi yao wenyewe. Takribani chaguzi 19 za urais au uchaguzi mkuu zimepangwa kufanyika katika bara hilo mwaka wa 2024, na hivyo kuashiria changamoto zaidi kwa AU.

Umoja wa Afrika | Addis Ababa Ethiopia
Wakuu wa mataifa ya Afrika watakutana Addis Ababa kuanzia Jumamosi katika mkutano wao wa kilele wa kila mwaka.Picha: Tony Karumba/AFP

Juhudi za kuzuwia mzozo juu ya uenyekiti

Umoja huo umeweza kuepusha mzozo kwa kutuliza mvutano kabla ya mkutano wa kilele kuhusu uenyekiti wa zamu wa mwaka mmoja wa AU, unaoshikiliwa na Rais wa Comoro Azali Assoumani.

Urithi huo ulikuwa umezuiwa kwa muda mrefu na mzozo kati ya Morocco na Algeria, vigogo wa eneo la Afrika Kaskazini ambao wadhifa huo unaangukia mwaka huu.

Soma pia: Ujumbe wa amani wa AU wakamilisha awamu mpya ya mpango wa kuondoka Somalia

Baada ya miezi kadhaa ya mazungumzo makali, Rais wa Mauritania Mohamed Ould Ghazouani anatarajiwa kuchukua nafasi ya uenyekiti.

Kipindi hiki kinaangazia mgawanyiko ndani ya shirika la Afrika nzima hata kama linatafuta kuwa na sauti yenye nguvu ndani ya kundi la G20 ambalo lilijiunga mnamo Septemba.  

Wachambuzi wanasema kuwa AU lazima ichukue hatua haraka ili kuendeleza maelewano ya jinsi ya kufanya biashara yake katika G20, ambayo inawakilisha zaidi ya asilimia 85 ya Pato jumla la dunia.  

Umoja wa Afrika | Macky Sall
Mkutano wa AU unafanyika katikati mwa mzozo mbaya wa uchaguzi nchini Senegal, ambapo Rais Macky Sall ameahirisha uchaguzi wa Februari hadi Oktoba na kuzusha machafuko.Picha: John Thys/AFP

Kwa kujiunga na G20, "AU itakuwa mhusika katika siasa za kimataifa," alisema Paul-Simon Handy, mkurugenzi wa kikanda wa Taasisi ya Mafunzo ya Usalama huko Addis Ababa. "Njia za kufanya kazi zitalazimika kupatikana haraka," alisema.

Solomon Dersso, mkurugenzi mwanzilishi wa tanki ya wanafikra ya Amani Africa, alikubali lakini akaonya kuwa mchakato huo "hautakuwa... rahisi". "Kama vile Umoja wa Ulaya, hii itahitaji kufanya mazungumzo ya mara kwa mara na maelewano," aliiambia AFP.

"Inakuwa ngumu zaidi unapokuwa na nchi 55 zenye maslahi tofauti, lakini haiwezekani."

Changamoto za AU

Lakini nafasi ya AU ya kufanya ujanja inaweza kuwa ndogo katika uso wa migogoro ya usalama inayolikabili bara la Afrika.

Afrika inakumbwa na ghasia mbaya katika eneo la Sahel, mapigano katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ambayo yamezua mvutano wa kidiplomasia wa kikanda, na migogoro nchini Somalia na Sudan.

Soma pia: Umoja wa Afrika wasema "umefadhishwa" na kujiondoa Niger, Mali na burkina Fasso ndani ya ECOWAS

"Nchi wanachama wanaangalia ndani, kulinda kwa karibu haki zao huru badala ya kuwekeza katika usalama wa pamoja," Shirika la Kimataifa la Migogoro lilisema katika maelezo mafupi kabla ya mkutano huo.  

Somo jingine kuu la mjadala linatarajiwa kuwa jinsi AU itakavyobadilika na kutegemea mataifa ya Afrika kufadhili sehemu kubwa ya bajeti yake badala ya wafadhili wa kigeni inayowategemea kwa sasa.  

Tangazo la kuahirishwa uchaguzi Senegal lazusha kizaazaa

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifamwezi Disemba lilipitisha azimio la kufadhili ujumbe wa amani unaoongozwa na AU, lakini likauweka katika asilimia 75 ya bajeti.

Mkutano huo "utalaazimika kutafakari juu ya athari" za kuongeza salio la bajeti, kulingana na Handy, hasa kwa nchi ambazo zimepeleka jumbe za kijeshi nje ya mfumo wa AU.